• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Kitendawili cha ‘dawa’ aina ya chai ya mitishamba kutibu Covid-19 Madagascar

Kitendawili cha ‘dawa’ aina ya chai ya mitishamba kutibu Covid-19 Madagascar

CHARLES WASONGA na MASHIRIKA

ANTANANARIVO, Madagascar

RAIS wa Madagascar Andry Rajoelina amependekeza matumizi ya ‘dawa’ aina ya chai ya mitishamba kwa wagonjwa wa Covid-19 nchini mwake.

Madai ya Rais Rajaelina kwamba ‘dawa’ hiyo, kwa jina Covid Organics (CVO), inayofanana na chai isiyo na maziwa, inawatibu wagonjwa wa Covid-19 yamevutia hisia mseto katika taifa hilo ambalo ni kisiwa kilichoko kilomita 400 kando ya pwani ya Afrika Mashariki.

Kufikia Ijumaa, Madagascar visa 128 vya maambukizi ya Covid-19 vilikuwa vimeripotiwa nchini Madagascar huku watu 82 wakiwa wamepona na hamna vifo vilivyotokea.

Hii ni kulingana na takwimu kutoka Chuo Kikuu cha Hopkin, Amerika, ambacho hunakili data kuhusu ugonjwa huo.

Kwenye ujumbe kupitia Twitter, Rajoelina amewataka raia wa Madagascar kuwa na imani kwa uwezo wa ‘dawa’ hiyo kulemea virusi vya corona.

Alisema faida yote kutokana na mauzo ya ‘dawa’ hiyo yataelekezwa katika Taasisi ya Utafiti ya Madagascar (MIAR).

“Majaribio yote yamefanywa na imebainika kuwa dawa hiyo inaweza kupunguza na hata kuondoa kabisa dalili za Covid-19 kwa wagonjwa wenye virusi vyake nchini Madagascar,” shirika la habari la Africanews lilimnukuu Rais Rejoelina akisema.

Lakini kwenye taarifa, Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) limeonya dhidi ya tiba kama hiyo likisema kufikia sasa halijaidhinisha tiba yoyote ya Covid-19.

Licha ya onyo hilo kutoka kwa WHO, idadi kubwa ya raia wa Madagascar wanafurika katika vituo ambako ‘dawa’ hiyo inasambazwa bila malipo, ingawa wengine bado wana tashwishi.

Rais Rajoelina ameamuru kuwa kinywaji hicho kisambazwe bila malipo kwa wananchi maskini na kiuzwe kwa bei nafuu kwa wananchi wengine.

Katika kipindi cha wiki moja iliyopita, hata wanajeshi wamekuwa wakitembea nyumba hadi nyumba kusambaza ‘dawa’ na CVO.

“Napendelea kunywa chai hii ya mitishamba ili niimarishe afya yangu. Vilevile, tangu zamani nimekuwa nikitumia dawa za kienyeji,” Josette, bibi – bikizee – mwenye umri wa miaka 60 anayeishi katika kitongoji cha Tsimbazaza jijini Antananarivo aliambia shirika la habari la Anadolu.

Maduka ya jumla na yale ya kuuza dawa jijini Antananarivo yameanza kuuza dawa ya CVO ambayo imepakiwa kwa chupa za kuanzia mililita 200 na zaidi. Na zinanunuliwa kwa haraka kwa sababu wateja ni wengi.

“Tulitaka kununua dawa hiyo. Lakini tulipoenda kwa duka la jumla lakini chupa za dawa hiyo zilikuwa zimeisha,” anasema Judith, mama wa mtoto mmoja. Ingawa hajaambukizwa virusi vya corona, ana hamu kubwa ya kuweka akiba ya dawa hiyo nyumbani kwake.

Taasisi ya Kutoa Mafunzo kuhusu Dawa Madagascar (ANAMEM) inasema imetambua uwezo wa dawa kama tiba ya virusi vya corona. Taasisi hiyo inatafakari kuanzisha mfumo wa kufuatilia hali ya watu waliotumia chai hiyo ya mitishamba.

Taasisi hiyo haipingi matumizi ya CVO na imewaachia wananchi kujiamulia kama wataitumia au la mradi wazingatie vipimo vilivyopendekezwa, haswa kwa watoto.

Rakoto Fanomezantsoa, mwanajeshi daktari na mkurugenzi mkuu wa Hospitali ya Soavinandriana, jijini Antananrivo, akisema kiungo kimoja cha CVO kinaimarisha kinga ya mwishi na hutokomeza virusi.

Dawa hiyo inatengenezwa kutoka na mmea kwa jina Artemesia Annua, kutoka China na kuingizwa nchini Madagascar katika miaka ya 1970s kwa ajili ya kutibu malaria.

Kufikia sasa, dawa hiyo inasambazwa katika maeneo matatu nchini humo, ambayo ni Analamanga, Haute, Matsiatra na Atsinanana ambayo yameandikisha visa vingi vya maambukizi ya virusi vya corona tangu Machi 19.

Kulingana na taarifa kutoka Afisi ya Rais wa Madagascar, mataifa matatu ya Afrika kama vile Senegal, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Guinea Bissau yamesaka maelezo kuhusu CVO.

Rais wa Senegal Macky Sall ameagiza dawa hiyo baada ya kuwasiliana na Rais Rejoelina, kulingana na vyombo vya habari nchini Senegal.

Kuna zaidi ya visa 33,000 vya maambukizi ya virusi vya corona, vifo 1,469 na jumla ya wagonjwa 10,152 waliopona katika mataifa 52 kati ya 54 bara Afrika, kulingana na Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Maganjwa Afrika.

You can share this post!

COVID-19: Kenya yathibitisha visa vipya 24 ikiwa idadi ya...

Watu 20 waponea kifo baada ya chombo cha majini kuzama Ziwa...

adminleo