• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 11:13 AM
COVID-19: Magoha abadili kalenda ya masomo

COVID-19: Magoha abadili kalenda ya masomo

Na CHARLES WASONGA

LIKIZO ya mwezi Agosti itafupishwa kwa majuma mawili, vipindi vya masomo kuendeshwa kwa saa nyingi na likizo fupi ya muhula wa pili kufupishwa kwa siku nne.

Hizi ni baadhi ya hatua ambazo Wizara ya Elimu inapanga kuchukua kukabiliana na athari za janga la Covid-19 kwa kalenda ya masomo shule zitapofungiliwa jinsi inavyotarajiwa Juni 2020.

Katika stakabadhi iliyowasilishwa kwa Kamati ya Bunge kuhusu Elimu, Wizara hiyo inasema kuwa hatua hizo ni baadhi ya mikakati ya kufidia muda ambao wanafunzi walipoteza baada ya mlipuko wa virusi vya corona.

Vilevile, mabadiliko hayo kwa kalenda ya masomo yanalenga kuwawezesha wanafunzi kukamilisha silabasi.

Waziri wa Elimu George Magoha alisema janga la Covid-19 limeathiri masomo ya wanafunzi 15 milioni katika shule za msingi, shule za upili lakini akaelezea matumaini kuwa mtaala wa masomo utakamilishwa.

“Tumefanya marekebisho kadhaa katika kalenda na masomo na hivyo tuko na imani kuwa walimu wetu watakamilisha silabasi kwa wakati,” Profesa Magoha akaeleza.

Hii ni ithibati tosha kuwa Serikali haina nia ya kuahirisha mitahani ya kitaifa ambayo imeratibiwa kufanywa mwishoni mwa mwaka 2020.

Kulingana na ratiba iliyotolewa na Baraza la Kitaifa la Mitahini (KNEC) Desemba 20, 2019, Mtihani wa Kitaifa wa Darasa la Nane (KCPE) unapasa kuanza Novemba 2 na kikamilishwa Novemba 3. Na Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KSCE) imepangiwa kuanza Novemba 7 na kukamilishwa rasmi mnamo Novemba 30.

Kumekuwa na hofu kuhusu hatima ya mitahani hiyo mlipuko wa virusi vya corona ulipochangia kufungwa kwa shule mnamo Machi 17, wiki tatum kabla ya kukamilika kwa muhula wa kwanza.

Hatua hiyo imesababisha watahiniwa kupoteza muda mwingi wa masomo ya kawaida ya darasani.

Japo, Wizara ya Elimu, kupitia Taasisi ya Kuandaa Mitaala Nchini (KICD) imekuwa ikiendesha vipindi vya masomo mitandaoni, redioni na kwenye runinga ya Edu TV, imebainika kuwa idadi kubwa ya wanafunzi, hasa kutoka jamii za kipato cha chini, wameachwa nje.

Vilevile, Wizara ya Elimu imesema kuwa ratiba ya masomo katika shule za kutwa za upili pia itafanyiwa mabadiliko ili vipindi vya masomo viendeshwe kwa saa nyingi.

Hii ina maana kuwa wanafunzi watahitajika kuripoti shuleni mapema na kurejea nyumbani kuchelewa, majira ya jioni.

“Sawa na sekta zingine nchini, Covid-19 imeathiri pakubwa sekta ya elimu ikiwemo ratiba ya masomo,” Profesa Magoha akasisitiza.

You can share this post!

Serikali yasema waliofurushwa Kariobangi walihadaiwa...

Wanaume wawili wakamatwa Mombasa kwa kujifanya maafisa wa...

adminleo