• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:10 PM
Wasiovalia barakoa wamulikwa na maafisa baadhi ya maeneo Nairobi

Wasiovalia barakoa wamulikwa na maafisa baadhi ya maeneo Nairobi

Na SAMMY WAWERU

MAAFISA wa polisi katika baadhi ya mitaa Nairobi walionekana ‘kuwamulika’ wakazi walioonekana bila barakoa.

Kisa cha kwanza cha maambukizi ya Covid-19 kiliporitiwa nchini Machi 2020, serikali ilitoa taratibu na maagizo jinsi ya kudhibiti maradhi hayo yasienee.

Uvaliaji barakoa hasa katika maeneo ya umma, ni mojawapo ya taratibu zilizoorodheshwa kuzuia maambukizi ya Covid-19, ugonjwa unaosababishwa na virusi hatari vya corona.

Mnamo Jumamosi, operesheni hiyo ya maafisa ilikuwa katika mtaa wa Kasarani, Roysambu na Zimmerman.

Maafisa wa polisi walionekana katika maeneo hayo mchana ambapo waliopatikana bila barakoa wakijipata pabaya.

“Tutachukulia hatua wasiojali hatari ya Covid-19 kwa kutovalia maski,” afisa mmoja akaambia umma eneo la Zimmerman.

Aidha, waliingia kwenye saluni, maduka, vinyozi na mikahawa kuona ikiwa utaratibu wa serikali ulikuwa unazingatiwa.

Walikuwa na gari lao kuwarahisishia usafiri wakiwa kazini.

Operesheni hiyo ililenga hasa kusambaratisha mikusanyiko ya watu.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi walilamika wakisema wanaitishwa hongo katika shughuli hiyo kwa wanaopatikana bila barakoa.

“Ni pesa tu wanakusanya na kuhangaisha raia,” akalalamika mkazi.

Wizara ya Afya imeripoti visa kadhaa vya maambukizi ya corona katika mtaa wa Kasarani, maafisa wa polisi wakitakiwa kuhakikisha wenyeji wanafuata taratibu na sheria zilizotolewa kuzuia usambaaji zaidi.

You can share this post!

Askofu akamatwa waumini wakitoroka Mikindani

Alenga kuisaidia Coast Stima ishiriki kipute cha KPL

adminleo