• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Legnano na Atalanta zathibitisha kifo cha kiungo chipukizi Andrea Rinaldi

Legnano na Atalanta zathibitisha kifo cha kiungo chipukizi Andrea Rinaldi

Na CHRIS ADUNGO

KIUNGO Andrea Rinaldi, ameaga dunia kutotakana na matatizo ya ubongo aliyoyapata wakati akishiriki mazoezi mepesi nyumbani kwake.

Matatizo hayo yalianza Ijumaa wiki jana.

Rinaldi aliwahi kuwa sehemu ya kikosi chipukizi cha Atalanta kwa kipindi kirefu na amewahi kuchezea kikosi cha Legnano katika soka ya daraja la chini nchini Italia. Baadhi ya vianzo kama shirika la Ansa vinasema amekuwa mali rasmi ya Legnano baada ya kununuliwa. Hata hivyo baadhi vimesema amekuwa huko kwa mkopo msimu huu.

“Ushawishi wake ulikuwa wa kuhisika uwanjani kila mara. Awe na mpira au la. Alifahamu jinsi ya kutangamana vyema na watu. Alipenda kila watu na akapendwa na kikosi kizima kwa kiwango sawa,” ikasema sehemu ya taarifa iliyotolewa na Atalanta.

Kwa upande wao, viongozi wa kikosi cha Legnano walisema, “Kifo cha Rinaldo kimetupiga pute johari adimu. Ametutoka ghafla na kutuachia pengo kubwa katika ulingo wa soka. Yasikitisha sana kifo chake kimekuwa cha kushangaza na kuondoka bila ya kuwaaga wenzake. Ni muhali sana kuamini au hata kufikiria kuwa hayuko nasi tena.”

Legnano ambao walithibitisha pia kiini cha kifo cha Rinaldi, walisema kwamba “sogora huyo aliwaarifu kwamba alikuwa hajihisi vizuri kwa kipindi cha siku tatu ila hapakuwa na lolote kubwa ambalo wangeweza kumfanyia.”

Vyombo vya habari nchini Italia viliripoti kwamba Rinaldo aliaga dunia akitibiwa katika hospitali ya Varese asubuhi ya Mei 11, 2020.

Rinaldi aliingia katika sajili rasmi ya Atalanta akiwa na umri wa miaka 13 pekee na akaichochea klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Italia (Serie A) kunyanyua ubingwa wa Super Cup kwa chipukizi wasiozidi umri wa miaka 17 mnamo 2016.

Aliwahi pia kuwajibikia vikosi vya Imolese na Mezzolara kwa mkopo kabla ya kutua Legnano aliowachezea katika jumla ya mechi 23 na kuwafungia bao moja msimu huu.

You can share this post!

ITABIDI MZOEE: Wakala afichua Ozil haondoki Arsenal hivi...

Madereva wa matrela wageuka wasambazaji wakuu wa corona

adminleo