• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
‘Chakula kinauzika sokoni kuliko bidhaa nyinginezo’

‘Chakula kinauzika sokoni kuliko bidhaa nyinginezo’

Na SAMMY WAWERU

BIASHARA ya chakula ndiyo inawaingizia wengi pesa kipindi hiki ambapo taifa linapambana kudhibiti maambukizi ya Covid-19.

Uchunguzi wa Taifa Leo katika masoko ya Jubilee na Migingo eneo la Githurai umebainisha kwamba wafanyabiashara wengi wameamua kuuza bidhaa za kula.

Hatua hiyo imetokana na biashara nyingi hasa zisizo za bidhaa za kula kudorora, athari zilizochangiwa na janga la corona ambalo limeathiri uchumi wa nchi na ulimwengu kwa jumla.

Baadhi ya wafanyabiashara Githurai tuliozungumza nao wamelazimika kufunga maduka, taswira inayoonyesha namna Wakenya wamepoteza nafasi za kazi katika kampuni, mashirika mbalimbali na hata kazi za wenyewe kujiajiri.

Waathirika wengi wamegeukia biashara ya bidhaa za kula kukidhi mahitaji ya kimsingi.

Eva Irungu alikuwa muuzaji wa nguo lakini sasa anasema ameamua kuuza ndizi.

“Kenya iliporipoti kuwa mwenyeji wa Covid-19, biashara ziliathirika pakubwa. Bidhaa za kula zinanunuliwa,” akaelezea Eva ambaye ni mama wa watoto wawili.

Anasema mumewe aliyefutwa kazi katika kampuni moja jijini Nairobi, sasa anauza vitunguu saumu katika soko la Marikiti.

Bw Samson Mukang’u aliyekuwa muuzaji wa viatu anasema alikuwa anapata hasara na hivyo ikamlazimu awazie biashara ya machungwa.

“Hata ingawa mapato si ya kuridhisha, yataniwezesha kukidhi mahitaji muhimu kwa familia yangu,” akasema.

Kiwango cha uchumi kimedorora kwa sababu ya athari za Covid-19, sekta ya juakali na inayochangia zaidi ya asilimia 75 ya nguvukazi nchini ikitajwa kuathirika kwa kiasi kikuu.

Wakenya wengi wanasema mapato wanayopokea kwa sasa ni ya kukimu riziki na mahitaji ya kimsingi.

“Biashara zinaanguka, mapato ninayopokea ni ya kula na kulipa kodi ya nyumba,” akasema Jack Muia, kinyozi eneo la Githurai.

Visa vya maambukizi ya virusi vya corona nchini vinaendelea kuongezeka, Wizara ya Afya ikihimiza umma kuzingatia taratibu na maagizo yaliyotolewa kudhibiti maambukizi.

You can share this post!

Serie A kurejelewa rasmi Juni 13

Alikosea wapi?

adminleo