• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 12:45 AM
Usambazaji wa vyakula vya msaada kwa walio karantini waanza Wajir

Usambazaji wa vyakula vya msaada kwa walio karantini waanza Wajir

Na FARHIYA HUSSEIN

KAUNTI ya Wajir imeanzisha shughuli ya ugavi wa vyakula kwa wakazi walioathirika na Ukimwi, walemavu na wale waliowekwa karantini kudhibiti Covid-19.

Akithibitisha, Gavana wa kaunti hiyo Bw Mohamed Abdi amesema lengo lao kuu ni kuhakikisha wale walio karantini wanapata vyakula vya kutosha.

“Tumenunua magunia 3,165 ya mahindi, vibuyu 1,819 vya mafuta ya kupikia na madebe 1,400 ya tende na vyote vitasambazwa kwa watu walio katika hali ngumu. Tunataka kuhakikisha katika msimu huu wa janga la korona na mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan watu wanapata msaada wa chakula,” gavana huyo akasema.

Shughuli hiyo ilianza Jumamosi na wale walio katika vituo vya karantini walipokea magunia 350 ya mahindi, vibuyu 90 vya mafuta ya kupikia na tende madebe 90.

Tangu kuzuka kwa ugonjwa wa Covid-19 nchini Kenya, Wajir ni miongoni mwa kaunti 23 kati ya 47 zilizoathiriwa na ugonjwa huo.

Kwa sasa kaunti hiyo imeripoti visa 15 huku watu 42 wakiwa katika vituo mbalimbali vya karantini.

“Hatuna vifo katika eneo letu na watu 15 walioambukizwa wako katika hali nzuri,” akasema Bw Abdi.

Makundi mengine ambayo yalilengwa katika msaada huo ni watu walio na Ukimwi, mayatima na watu walemavu.

“Tayari wale wanaoishi na ulemavu wamepokea magunia 100 ya mahindi, vibuyu 60 vya Mafuta ya kupikia na tende debe 80,” gavana huyo alisema.

Alizidi kusema kuwa tayari wametayarisha kikosi ambacho kitashughulika kuwakamata watu ambao wanapita kwenye mipaka ya kaunti hiyo na nchi ya Somalia.

“Katika maabara yetu hadi sasa sampuli 143 zimefanyiwa vipimo vya Covid-19 na wafanyakazi 31 wanaohudumu katika vituo mbalimbali vya karantini, na watu 27 walipimwa na wanasubiri matokeo ikiwemo wanne kutoka kambi ya wakimbizi ya Dadaab (Kaunti ya Garissa), na wawili kutoka Dobley nchini Somalia,” Bw Abdi alisema.

Kamishna wa Kaunti hiyo Jacob Narengo amewasihi wakazi waripoti wale wanaojaribu kuingia katika kaunti hiyo kupitia njia zisizokubalika.

“Mipaka yetu na nchi ya Somalia inaendelea kutuweka katika hatari ya maambukizi. Tunapaswa kuendelea kuwa macho kila wakati. Nawasihi muwe salama katika nyumba zenu,” Bw Narengo akasema.

You can share this post!

IEBC yaanika uozo wake

Ukarabati wa barabara za lami waendelea Kiambu

adminleo