• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
KURUNZI YA PWANI: Elungata aelezea Wapwani haja ya kushirikiana na maafisa maeneo mpakani yasalie salama

KURUNZI YA PWANI: Elungata aelezea Wapwani haja ya kushirikiana na maafisa maeneo mpakani yasalie salama

Na WINNIE ATIENO

MSHIRIKISHI wa eneo la Pwani Bw John Elungata na afisa wa uhamiaji Bi Jane Nyandoro wamewaonya wakazi wanaoishi mipakani dhidi ya kuwaruhusu raia wa kigeni kuingia humu nchini kiharamu.

Aidha wamewataka wakazi hasa wa Kwale kuwataarifu maafisa wa usalama kila wanapoona raia wa kigeni wakiingia nchini kwa njia za mkato.

Bw Elungata alisema yeyote anayeingia humu nchini atatakiwa kuwekwa kwenye karantini.

Akiongea huko Kwale, Bw Elungata alisema mtu yeyote anayeingia humu nchini atapimwa ibainike hali yake kiafya hasa ikiwa ana virusi vya corona au la.

“Lakini tunachosema ni kwamba kama unatoka Tanzania, Msumbiji au nchi yoyote ile na unakuja Kenya, lazima upitie sehemu fulani upimwe na ukipatikana una ugonjwa wa Covid-19 unaweza kurudi kwenu. Lakini kama unaingia kwetu lazima uwekwe karantini ukimaliza muda wako unaendelea na shughuli zako,” alisema Bw Elungata.

Hata hivyo, alibainisha kwamba Kenya na Tanzania hazina mgogoro.

Bw Elungata alisema wageni 66 walitiwa mbaroni na polisi walipokuwa wakijaribu kuingia humu nchini wakitumia njia za mpenyo – panya routes – na kuwekwa kwenye karantini.

“Walipomaliza waliachiliwa na kurudi makwao. Tunajua wazee wa mitaa Lunga Lunga wanafanya kazi nzuri sana. Kama kuna ndugu zetu wengine ambao wanashawishika kuwavusha watu, tusiwakubalie kwa sababu ni hatari,” akasema.

Imefichuka kwamba baadhi ya raia wa Tanzania wanaingia humu nchini kupitia Bahari Hindi wakivuka kwa kutumia ngalawa au maboti.

Hata hivyo, Bw Elungata alisema maafisa wa polisi wakishirikiana na wale wa kuchunga bahari – Kenya Coast Guard – wataendelea kushika doria kuhakikisha hakuna raia wa kigeni wanaingia nchini kiharamu.

Aliwaonya wakazi wa Kwale dhidi ya kuwavukisha raia wa Tanzania hadi nchini akisema ni hatari.

“Kuna mtu ambaye anafanya kazi ya kuwaleta Watanzania, usiku wa manane anawatoa, nitamwambia kamishna wa kaunti amkamate na ampeleke karantini. Labda hata kwake kuna mtu amepata ugonjwa,” alisema

Bw Elungata alisema yeyote anayetoroka katika kituo cha karantini katika kaunti za Mombasa, Kwale ua Kilifi, aliyekaa na mgeni ambaye hajamtambulisha na yule aliyekataa kwenda karantini wote watatiwa mbaroni.

“Hatuna shida na hatung’ang’anii mpaka bali tunapigana na ugonjwa pekee. Mtu kama anakuja Kenya na anatoka Tanzania, hatuna shida na yeye sisi ni watu wa Afrika Mashariki tuna mikataba, tunafanya mikakati yetu pamoja hatuna matatizo,” akasema.

Amewataka maafisa wanaolinda mipaka ya Kenya kuwa makini na kuhakikisha watu wanaopita ni wale wanaotakiwa au wanaingia kihalali.

Lakini akasema wazi katika kipindi hiki kigumu ni mizigo pekee ndiyo inayotakiwa kuingia nchini kuepusha watu kutangamana kwa wingi.

Naye afisa wa uhamiaji Bi Nyandoro akasisitiza haja ya kuwakamata wanaotumia njia za kujifichaficha.

“Mkiona watu wanatumia njia za konakona kuingia Kenya tafadhali tujulishe. Tumekwua tukishirikiana na vyombo kadhaa vya usalama kuwakamata wale wanaoingia Kenya kwa njia za mpenyo. Lazima tujilinde,” akasema Bi Nyandoro.

You can share this post!

Wazee wa Agikuyu wasambaza chakula kwa waathiriwa eneo la...

TANZIA: Nyota wa zamani wa timu ya taifa raga Allan Makaka...

adminleo