• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 11:55 AM
Shujaa yavunja ndoa na kocha Paul Feeney

Shujaa yavunja ndoa na kocha Paul Feeney

Na CHRIS ADUNGO

SHIRIKISHO la Raga la Kenya (KRU) limeanzisha mchakato wa kutafuta kocha mpya wa timu ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande, Shujaa.

Hii ni baada ya KRU kukatiza uhusiano na mkufunzi mzawa wa New Zealand, Paul Feeney aliyevunja rasmi ndoa kati yake na shirikisho hilo mwishoni mwa Aprili 2020.

Kutamatika kwa uhusiano wao kulikuwa ni zao la maafikiano kati ya KRU na Feeney aliyewaongoza Shujaa kutia kibindoni ubingwa wa Raga ya Afrika kwa upande wa wanaume.

Ushindi huo uliwakatia Shujaa tiketi ya kufuzu kushiriki makala ya 32 ya Michezo ya Olimpiki yatakayoandaliwa jijini Tokyo, Japan mnamo 2021 baada ya kuahirishwa kwa kipindi cha mwaka mmoja zaidi kutokana na janga la corona.

Feeney aliyewahi kudhibiti mikoba ya timu ya taifa ya Fiji mnamo 2015, pia aliiongoza Kenya Morans kutinga fainali ya Tusker Safari Sevens mnamo 2019 japo alishindwa kuongoza Shujaa kukamilisha duru za Raga ya Dunia zilizositishwa kwa sababu ya ugonjwa wa Covid-19.

Shujaa wanatazamiwa kurejea ulingoni kunogesha duru nne za mwisho za Raga ya Dunia msimu huu jijini London na Paris mnamo Septemba kabla ya kutua Singapore na Hong Kong mnamo Oktoba, 2020.

Feeney aliondoka Kenya kuelekea New Zealand kujumuika na familia yake baada ya kushikilia mikoba ya Shujaa na Morans kwa kipindi kifupi.

Kwa mujibu wa KRU, Feeney kwa sasa hawezi kurejea humu nchini kutokana na kanuni mpya zinazodhibiti safari za ndege za kimataifa kutokana na Covid-19.

“Mchakato wa kuziba pengo lililotokana na kuondoka kwake umeanza na yeyote anayeazimia kuzingatiwa kwa nafasi hiyo yuko huru kutuma maombi ya kazi,” ikasema sehemu ya taarifa ya KRU.

“KRU ingependa kumshukuru Feeney kwa mchango wake katika makuzi ya raga yetu kwa kipindi alichohudumia timu ya taifa. Tunamtakia kila la heri katika shughuli zake za baadaye,” ikaongeza taarifa hiyo.

Feeney aliteuliwa kuwa kocha wa Shujaa mnamo Septemba 2019 baada ya mkataba wa Paul Murunga kutamatika.

Chini yake, Kenya Morans walinyakua ufalme wa Safari Sevens mnamo 2019 huku Shujaa wakiridhika na nishani ya shaba katika mashindano hayo yaliyonogeshwa pia na Ufaransa, Afrika Kusini, Amerika, Uhispania, Ureno, Namibia na Hong Kong.

Ingawa hivyo, matokeo ya Shujaa katika Raga ya Dunia hayajakuwa ya kuridhisha zaidi chini ya Feeney hasa ikizingatiwa kwamba kwa sasa wanashikilia nafasi ya 12 kwa alama 35 baada ya kutandaza duru sita katika kivumbi hicho cha duru 10.

Feeney amewahi pia kunoa vikosi vya raga vya Auckland na Stormers nchini New Zealand na Afrika Kusini mtawalia.

You can share this post!

Juventus waingia fainali ya Coppa Italia licha ya Ronaldo...

Bajeti Kuu yatenga Sh1.7 bilioni kwa barabara za Kiambu

adminleo