• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Mbunge ataka maafisa wasihujumu uchunguzi chakula kilichodhuru kadhaa Kikuyu

Mbunge ataka maafisa wasihujumu uchunguzi chakula kilichodhuru kadhaa Kikuyu

Na MWANGI MUIRURI

MBUNGE wa Kikuyu Kimani Ichung’wa ameteta kwamba kuna maafisa wakuu serikalini katika idara za kiusalama wanaohujumu uchunguzi kuhusu kisa ambacho wakazi wa eneobunge lake walipewa chakula chenye madhara kiafya.

Chakula hicho kilikuwa kimetolewa zaidi ya wiki mbili zilizopita kama cha msaada na ambapo kiliishia kuwaathiri wahanga kwa kuwatwika shida za kiafya na kuishia kulazwa hospitalini.

Bw Ichung’wa anadai maafisa hao ambao hakuwataja wanacheza siasa na kisa hicho ambacho hakikuwa na utu kamwe na kilichowaathiri watu 19.

“Chakula hicho kilipeanwa katika mtaa wa Gikambura na ambapo kilikuwa kimebandikwa majina ya mimi kama mbunge na pia lile la wakfu wa Dkt William Ruto akiwa ndiye naibu wa rais. Njama ilikuwa sisi wawili tuibuke kama waovu wa kudhuru watu wa Gikambura kwa chakula na hivyo basi tupoteze umaarufu wa kisiasa,” akasema.

Waliokisambaza chakula hicho alisema ni wa mrengo pinzani wa kisiasa na ambao nia yao kuu ni kumpotezea DP Ruto umaarufu katika eneo hilo la Gikambura na kitaifa.

Mbunge huyo aliteta kuwa hadi leo hii, hakuna lolote la kuwakamata waliohusika limetekelezwa na wachunguzi “licha ya kwamba tumetoa habari muhimu kuhusu kisa hicho kama nambari za usajili wa magari ambayo yalitumika pamoja na maelezo ya umbo na sura za waliosambaza chakula hicho”.

Chakula hicho kilisambazwa muda mfupi baada ya mbunge huyo na Dkt Ruto kutoa msaada wao wa chakula kupitia kwa wachungaji ambao walikongamana katika mji wa Kikuyu na kupewa misaada hiyo wawasilishe kwa waumini wao waliokuwa katika hali ya njaa kupitia mkurupuko wa maradhi ya Covid-19.

Alidai kuwa amepokezwa habari muhimu na baadhi ya maafisa wa polisi kwamba “kuna ilani zimetolewa tusithubutu kuwakamata waliohusika wala kuwaanika kwa umma kwa kuwa wako na ushawishi mkuu wa kisiasa na kiserikali”.

Ichung’wa alisema kuwa licha ya kuwa barabara ambazo zilitumika na wasafirishaji wa chakula hicho zimepambwa na kamera za siri za kiusalama na ambazo zilinakili mienendo ya wahaini hao, kuna maafisa ambao wamezitwaa picha hizo na kuzikatalia katika makao makuu ya polisi, Nairobi.

“Wametoa tu ilani kwa maafisa nyanjani wasahau kuwa kuna mikanda hiyo ya kamera na wakiulizwa waseme haikunakili lolote au chochote kama ushahidi wa kutatua kisa hicho,” akasema Bw Ichung’wa.

You can share this post!

Sato Tap, ubunifu wa kisasa wa kunawa mikono

VINYWAJI: Jinsi ya kutayarisha sharubati ya mananasi

adminleo