• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
Mmoja apata majeraha baada ya kuhusika katika ajali Thika Road

Mmoja apata majeraha baada ya kuhusika katika ajali Thika Road

Na SAMMY WAWERU

WATU watano walinusurika kifo katika ajali iliyotokea Jumatano jioni katika barabara ya Thika Superhighway.

Ajali hiyo iliyotokea eneo la Clayworks, kati ya Roysambu na Githurai, ilihusisha magari mawili ya kibinafsi.

Akithibitisha mkasa huo, afisa mmoja wa trafiki anayehudumu Thika Road alisema mtu mmoja alipata majeraha.

“Gari moja lilikuwa na watu wawili na lingine watatu, mmoja miongoni mwao alipata majeraha na amepelekwa hospitalini,” afisa huyo akasema.

Aidha, ajali hiyo ilifanyika katika leni ya kasi, na kulingana na afisa huyo wa trafiki uchunguzi umeanzishwa kubaini kiini.

Hata hivyo, kwa mujibu wa maelezo ya mmoja wa manusura na aliyekuwa katika gari lililokuwa mbele, alimokuwa liligongwa kutoka nyuma. “Liliendeshwa kwa mwendo wa kasi, na ni kwa neema ya Mungu tumenusurika kifo,” alieleza.

Ajali hiyo imetokea majuma kadhaa baada ya nyingine kufanyika mita kadhaa kutoka eneo la tukio la Jumatano.

Mnamo Juni 13, 2020, watu watatu waliponea kifo kwa tundu la sindano baada ya lori la kusafirisha kokoto na vifaa vya ujenzi, walimokuwa, kupoteza mwelekeo likiwa katika leni ya kasi, likang’oa vyuma vya kando ya barabara na kuanguka katika mtaro wa majitaka ulio kati ya leni ya kasi na ya nje inayotumika kuchukua na kushusha abiria.

Visa vya ajali Thika Superhighway vinaendelea kuongezeka, uendeshaji wa magari kwa kasi na ubadilishaji leni bila uangalifu vikitajwa kama visababishi vikuu.

Pia, eneo kati ya Roysambu na Githurai, limeanza kumulikwa kutokana na ajali za mara kwa mara.

You can share this post!

Waiguru adai msimamo wake kuunga BBI ndiyo sababu ya...

Real Madrid warejea kileleni mwa La Liga katika gozi...

adminleo