• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Raila atangaza mwisho wa ‘Resist’

Raila atangaza mwisho wa ‘Resist’

Na BENSON MATHEKA

KIONGOZI wa upinzani, Raila Odinga, Jumanne alitumia sherehe za Leba Dei za mwaka huu, kusitisha marufuku ya wafuasi wake ya kutotumia bidhaa za kampuni ambazo muungano wa NASA ulidai zilisaidia serikali ya Jubilee kuvuruga uchaguzi mkuu 2017.

Alisema marufuku hiyo ilichangia kudorora kwa uchumi na kwa sababu amekubali kushirikiana na serikali, hakuna haja ya kuendelea kususia bidhaa za kampuni hizo.

“Tuliwaambia mkome kutumia bidhaa za Safaricom, Brookside, Bidco na Haco miongoni mwa kampuni nyingine kwa sababu zilikuwa zikisaidia serikali ya Jubilee.

Sasa kwa sababu Rais Kenyatta alinitafuta na mimi nikamtafuta na tukakutana na kuzungumza, ninawaambia endeleeni kutumia bidhaa za kampuni hizo,” alisema Bw Odinga.

Ilikuwa mara yake ya kwanza kurudi Uhuru Park tangu kuapishwa kwake kama rais wa wananchi Januari 30 mwaka huu.

Alisisitiza kuwa muungano wa NASA ungali imara licha ya tofauti kuzuka baada ya kujiapisha na kusalimiana na Rais Kenyatta. “NASA iko na ingali imara. Mnaniona hapa na Musalia Mudavadi. Kalonzo Musyoka na Moses Wetangula pia wametuma salamu zao,” alisema.

Kwenye sherehe za jana viongozi wa vyama vya wafanyakazi na waajiri walitumia fursa hiyo kuitaka serikali kusitisha mabadiliko ya sheria za Leba.

Wakihutubu katika bustani ya Uhuru Park ambako sherehe hizo ziliandaliwa, viongozi hao walisisitiza kuwa mabadiliko hayo yananuiwa kunyima wafanyakazi haki zao za kikatiba na hawatayakubali.

“Wafanyakazi wamekataa mabadiliko yoyote ya kisheria ambayo yanalenga kuwanyima haki zao za kikatiba. Tunasema kwamba hatutakubali,” alisema Katibu Mkuu wa Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi nchini (Cotu) Bw Francis Atwoli. Aliwataka wabunge kukataa mabadiliko hayo yakiwasilishwa mbele yao.

Katibu Mkuu wa chama cha walimu Wilson Sossion alisema wafanyakazi hawatakubali wawakilishi wao kuondolewa katika bodi za NSSF na NHIF.

 

You can share this post!

Gathimba kuwania mamilioni Matembezi ya Dunia Uchina

Serikali yawazia kuzuia matumizi ya mafuta taa

adminleo