• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Kisumu All Stars wakatiza uhusiano na kipa chaguo la kwanza

Kisumu All Stars wakatiza uhusiano na kipa chaguo la kwanza

Na CHRIS ADUNGO

KIKOSI cha Kisumu All Stars kimethibitisha kwamba kimeagana rasmi na kipa chaguo la kwanza Gad Mathews baada ya mkataba wake kutamatika.

Afisa Mkuu Mtendaji wa klabu hiyo, Nicholas Ochieng amesema All Stars wanalenga pia kukatiza uhusiano na wanasoka sita zaidi. Gad, 24, alisajiliwa na All Stars mnamo Januari 2020 kwa kandarasi ya miezi sita na akapata uhakika wa kuunga kikosi cha kwanza.

Kipa huyo wa zamani wa Wazito FC, tayari anahusishwa na uwezekano mkubwa wa kusajiliwa na Tusker FC au kurejea kambini mwa Kariobangi Sharks.

All Stars wanatarajiwa kupepetana na Vihiga United waliomaliza kampeni za NSL katika nafasi ya tatu kubaini kikosi cha tatu kitakachoshuka daraja kwenye KPL na kitakachopanda ngazi kutoka NSL kwa minajili ya kinyang’anyiro cha msimu ujao wa 2020-21.

Kwingineko, Western Stima wapo katika hatari ya kuagana na wanasoka wao wa haiba kubwa kutokana na uchechefu wa fedha ambao umechangiwa na hatua ya kampuni ya Kenya Power kusitisha udhamini wao.

Vikosi vingi vya haiba katika Ligi Kuu ya Kenya (KPL) sasa vinamezea mate masogora wa Stima walioridhisha zaidi katika kampeni za msimu uliopita kwa matumaini ya kuchuma nafuu kutokana na hali mbovu ya kifedha ya waajiri wao na hatimaye kuwasajili.

Kati ya wachezaji wanaotarajiwa kukatiza uhusiano wao na Stima ni Kelly Wesonga, Fidel Origa, Maurice Ojwang na mfumaji chipukizi wa Harambee Stars, Benson Omalla.

Ingawa hivyo, mwenyekiti Laban Jobita amesisitiza kwamba uthabiti wao hautayumbishwa na tukio hilo kwa kuwa wanapania kujishughulisha vilivyo katika soko la uhamisho baada ya muhula wa usajili wa wachezaji kufunguliwa rasmi.

“Tuna mpango wa kujinasia maarifa ya chipukizi wengi watakaoongoza kampeni zetu zijazo. Stima haitamkwamilia mchezaji yeyote anayeazimia kutafita hifadhi mpya kwingineko,” akatanguliza kinara huyo kwa kusisitiza haja ya klabu zinazovizia wanasoka wa Stima kuzingatia taratibu zilizopo za kusajili wachezaji.

“Wote wanaotaka kuagana nasi wako huru kufanya hivyo ila kwa kuzingatia taratibu zote zilizopo. Sera zetu haziwezi kuturuhusu kumkwamilia mchezaji ambaye anahisi atapiga hatua kubwa kitaaluma akivalia jezi za kikosi kingine ispokuwa Stima,” akasema Jobita.

Jobita ambaye ni mwanasoka wa zamani wa Gor Mahia na Kisumu Hotstars, amefichua kuwa mikakati ya Stima kwa sasa ni kutafuta mdhamini mpya na kutathmini maombi ya wanasoka wengi wanaotazamia kujiunga nao kabla ya kuanza mchakato wa kusajili wanafunzi wa shule za upili na vyuo kwa minajili ya msimu ujao wa KPL.

You can share this post!

Manchester City yapewa idhini ya kuvaana na Real Madrid...

Manchester City waponea adhabu baada ya CAS kubatilisha...

adminleo