• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 2:08 PM
Pigo kwa walevi sheria mpya ikipitishwa

Pigo kwa walevi sheria mpya ikipitishwa

Na VALENTINE OBARA

WALEVI na wafanyabiashara za vileo watapata pigo iwapo serikali itatekeleza pendekezo la kupiga marufuku unywaji wa pombe katika mikahawa.

Sheria mpya iliyopendekezwa na Wizara ya Afya, inataka mtu yeyote anayefanya biashara ya kuuza pombe, iwe ni katika mikahawa au madukani, ahakikishe wanunuzi hawanywi mahali hapo.

Ni sheria ambayo imelenga kupunguza ueneaji wa virusi vya corona, hasa baada ya kubainika kuwa kuna wafanyabiashara wa mikahawa ambao walitumia vibaya nafasi waliyopewa kuuza vyakula.

Kanuni zilizopo kwa sasa zinaruhusu watu kunywa pombe katika mikahawa wakati wanapokula, lakini imebainika hili lilitoa mwanya kwa watu kulewa bila kufuata masharti ya kujikinga kutokana na Covid-19.

Mkuu wa Afya ya Umma, Dkt Francis Kuria, alithibitisha wizara ilibuni pendekezo hilo jipya ambalo sasa linasubiri kuidhinishwa na Mwanasheria Mkuu.

‘Sheria hiyo inalenga kutatua changamoto zinazohusu unywaji wa pombe. Itakapopitishwa ndipo tutaweza kuijadili kwa mapana zaidi,’ akasema Dkt Kuria.

Katika mapendekezo hayo, mtu yeyote atakayekiuka sheria hizo atatozwa faini isiyozidi Sh20,000 au atumikie kifungo kwa miezi sita.

Alisema hayo katika kikao cha wanahabari kuhusu hali ya virusi vya corona nchini.Waziri Msaidizi wa Afya, Dkt Rashid Aman, alitangaza kuwa idadi ya maambukizi iliongezeka kwa 397 na kupelekea idadi jumla kuwa 14,168.

Wagonjwa 642 walipona, na hivyo kufikisha jumla ya waliopona hadi 6,258. Hata hivyo, wengine 12 walifariki na kufikisha idadi yao hadi 250.

You can share this post!

Wiper yavunja mkataba na Nasa, yaingia Jubilee rasmi

Matumaini ya mavuno licha ya janga la corona

adminleo