• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
Kajembe apumzishwa kwa kanuni za corona

Kajembe apumzishwa kwa kanuni za corona

Na MOHAMED AHMED

ALIYEKUWA mbunge wa Changamwe, Ramadhan Seif Kajembe alizikwa jana katika maziara ya Kwa Shee eneo la Jomvu katika hafla ambayo ilitamatisha safari ya mkongwe huyo wa siasa.

Mazishi hayo yalifanywa kwa msingi wa sheria za kudhibiti uenezaji virusi vya corona, kwa usimamizi wa maafisa wa afya waliobeba mwili hadi kaburini.Kwa msingi huu, mazishi yake yaliyohudhuriwa na watu wachache yalitofautiana na maisha yake ya kisiasa ambapo alikuwa akizingirwa na watu wakati mwingi.

Bw Kajembe ni miongoni mwa viongozi wa Pwani waliohudumu kwa miaka mingi zaidi, akiwa na miaka 30 uongozini.Ndani ya miaka hiyo, Bw Kajembe aliyefariki Ijumaa akiwa na miaka 76 alihudumu kama mbunge wa eneo la Changamwe kwa miaka 15 na miaka mengine 15 akahudumu kama diwani wa eneo la Mikindani.

“Kila uchaguzi ukija mimi nilikuwa nikienda kuwaaga wenzagu ambao walikuwa miongoni mwa wabunge 21 kutoka Pwani kwa maana kati yao ni watano ama sita ndio walikuwa wanapata fursa ya kurudishwa mamlakani na mimi nilikuwa miongoni mwao,” akasema Bw Kajembe katika mahojiano ya mwaka jana katika runinga.

Bw Kajembe alianza siasa kama kijana katika chama cha Kanu mwaka 1960 kabla kuingia kwenye nafasi ya udiwani wa Mikindani aliyoishikilia kwa miaka 15.

Kuanzia mwaka wa 1997, Bw Kajembe alishinda kiti cha ubunge kupitia tiketi hiyo ya KANU na kushinda tena katika uchaguzi wa 2002 na 2007 kupitia tiketi ya chama cha NARC na cha ODM mtawalia.

“Uwezo wake wa kuelewana na watu ndio ulimuezesha kuweza kupewa nafasi kwa muda mrefu. Tulikuwa na yeye bungeni na mimi nilipoondoka yeye bado akaendelea kwenye nafasi hiyo na kuhudumia watu wake,” akasema aliyekuwa mbunge wa Likoni Rashid Shakombo.

Bw Kajembe alijisifia kuwa miongoni mwa viongozi walionzisha chama cha ODM wakiongozwa na Raila Odinga.Kwa upande wa maendeleo, alikuwa miongoni mwa viongozi ambao walipigania kugawanywa kwa eneo bunge la Changamwe na kupelekea kuzaliwa kwa eneo bunge la Jomvu.

Alijitaja pia kupigania kuzaliwa kwa kata ndogo za Kipevu na Airport ili kupeleka huduma karibu na wananchi.Aidha, upande wa elimu Bw Kajembe alijivunia kuanzisha ujenzi wa shule tatu za upili ikiwemo shule ya upili ya Kajembe, shule ya upili ya wasichana ya Jomvu na shule ya upili ya Miritini.

Bw Kajembe ambaye pia alikuwa mwanachama wa wafanyabiashara alipigania haki za wafanyabiashara na vijana kwa kuwasaidia kwa mahitaji mbalimbali.

Mwaka 2013, Bw Kajembe ambaye pia aliwahi kuhudumu kama naibu waziri wa mazingira alijaribu bahati ya kuwania kiti cha useneta lakini akashindwa na aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar.

Baadaye mwaka 2016 akateuliwa na Rais Uhuru Kenyatta kuwa mwenyekiti wa bodi ya shirika la huduma za feri (KFS) kwa muda wa miaka mitatu.

Wakati wa uongozi wake huo KFS, Bw Kajembe alisaidia kuzuia mabwenyenye kunyakua ardhi inayomilikiwa na shirika hilo na pia akapokea feri ya Mv Jambo ambayo ni miongoni mwa zile mpya ambazo zilinunuliwa kwa gharama ya Sh2 bilioni.

Kajembe alifariki katika hospitali ya Pandya ambapo alikuwa amelazwa. Kifo chake kilitokea wiki chache baada ya kufariki kwa mkewe wa kwanza Aziza ambaye miezi minne baada ya yule wa pili Zaharia.

Jana, miongoni mwa viongozi waliokuwa hapo ni pamoja na mshirikishi wa kanda ya Pwani John Elungata, naibu kamanda wa polisi wa Mombasa Joseph Chebii, mbunge wa Jomvu Badi Twalib ambaye ameoa mtoto wa marahemu pamoja na kiongozi wa wengi katika bunge la Mombasa Hamisi Mwidani ambaye pia ni jamaa yake marehemu.

Bw Elungata alisoma risala ya rambi rambi za Rais Uhuru Kenyatta ambaye alimtaja Bw Kajembe kuwa kiongozi mwenye maono na anayefaa kuigwa.

Naibu Rais William Ruto kiongozi wa ODM Raila Odinga Gavana wa Mombasa Hassan Joho na Seneta Mohammed Faki pia walitoa rambi rambi zao kwa marehemu na kumtaja kielelezo chema.

You can share this post!

Ngome ya Ruto yapasuka vipande vitatu

Maseneta wanavyotumia utata wa ugavi wa mapato kujijenga

adminleo