• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:50 AM
‘Tangatanga’ wakiri fimbo ya Uhuru yatisha

‘Tangatanga’ wakiri fimbo ya Uhuru yatisha

Na ONYANGO K’ONYANGO

WANDANI wa Naibu Rais William Ruto, wamekiri kuwa fimbo kali ya Rais Uhuru Kenyatta iliwalazimu kuenda chini ya maji.

Kwa miezi kadhaa sasa, wafuasi hao wa kikundi hiki maarufu kama Tangatanga wamepunguza shughuli zao za kisiasa baada ya msururu wa adhabu kutoka kwa wakuu wa Chama cha Jubilee wanaomtii Rais Kenyatta.

Miongoni mwa adhabu walizopewa ni kupokonywa nyadhifa muhimu bungeni, huku wengine wakidai kuandamwa na asasi za usalama serikalini.

“Ukiamua kufanya jambo ambalo linakinzana na Rais, unatishwa kwamba watakupeleka kwa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kuchunguza vile unavyotumia Hazina ya Kustawisha Maeneobunge (NG-CDF),” akasema Naibu Katibu Mkuu wa Jubilee, Caleb Kositany, aliye mwandani mkubwa wa Dkt Ruto.

Majuzi, Dkt Ruto aliwarai viongozi wa makanisa kuwaombea washirika wake, akisema baadhi yao wanatishwa kufikishwa mahakamani ikiwa hawatafuata mielekeo fulani ya kisiasa.

Licha ya wengi wao kuamua kukaa kimya, Mbunge wa Keiyo Kusini, Daniel Rono, alisema baadhi yao hawafurahishwi na hali hiyo.

“Rais Kenyatta ana udhibiti kamili wa serikali, hivyo Dkt Ruto hawezi kumkabili jinsi baadhi yetu tunavyotaka. Vilevile, (Ruto) anamheshimu Rais, hivyo hawezi kufanya jambo lolote linaloonyesha wazi anamkosea heshima mkubwa wake,” akasema Bw Rono.

Wanachama wa Jubilee wanaoegemea upande wa Rais walisema wandani wa Dkt Ruto wako kwenye njiapanda, hivyo hawapaswi kudai Rais anawakandamiza.

Mbunge wa Cherangany, Bw Joshua Kuttuny, alisema kuwa ni dhahiri sasa washirika wa Dkt Ruto wamepoteza mwelekeo kisiasa kwani hawakutarajia mbinu ambazo Rais alitumia ‘kuilainisha’ Jubilee baada yao kumkosea heshima kwa muda mrefu.

“Wanapaswa tu kukubali kwamba wameshindwa,” akasema Bw Kutuny.

Kwa mujibu wa mbunge wa Nyeri Mjini, Ngunjiri Wambugu, huenda ikawa Tangatanga wameshindwa katika mbio zao, na sasa wameamua kunyamaza kwa muda ili kujipanga upya.

You can share this post!

Waliovuna enzi za Moi wasota

Phil Jones kukosa kampeni zilizosalia za Manchester United...

adminleo