• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
Mbunge wa Thika awatetea wakandarasi

Mbunge wa Thika awatetea wakandarasi

Na LAWRENCE ONGARO

WANANCHI wamehimizwa kutoka maoni yao kuhusu mswada wa zabuni uliowasilishwa bungeni wa mwaka 2020 na ambao unapendekeza aliyepewa kazi na serikali alipwe haki yake bila kucheleweshwa.

Mbunge wa Thika Bw Patrick ‘Jungle’ Wainaina akihutubia waandishi wa habari mjini Thika mnamo Jumanne, alisema tayari amewasilisha mswada bungeni wa kutaka serikali kuu na za kaunti zifanye haki kwa kuwalipa haki yao wakandarasi wanaopewa zabuni ya kufanya kazi yoyote ile.

“Tayari mswada huo uko katika awamu ya kwanza ambapo bado unaendelea kujadiliwa na wabunge,” alisema Bw Wainaina.

Mbunge huyo ambaye ndiye aliwasilisha mswada huo bungeni ili safu hiyo iujadili kikamilifu, alisema wananchi pia wana nafasi ya kutoa maoni yao kabla ya mswada huo kupelekwa katika awamu ya pili.

Kulingana na mbunge huyo, ni vyema kuwa na ushirikiano wa serikali na benki za humu nchini ambapo iwapo serikali itachelewa kulipa makontrakta fedha zao walizofanyia kazi, kwa muda wa siku 90, basi inabidi wahusika waende katika benki na kupokea fedha zao ili serikali ilipe benki baadaye deni hilo.

“Mpango huo kulingana na maoni yetu ni wa kuridhisha kwa sababu wale waliopewa zabuni na serikali watapata afueni ya kupokea haki yao bila kucheleweshwa jinsi hali ilivyo sasa,” alisema mbunge huyo.

Alisema sababu kuu ya kutetea hali hiyo ni kuwa, watu wengi waliopewa kazi na serikali huchelewa kupewa haki yao na hivyo kusababisha wengine kuuza mali zao baada ya kukosa namna.

“Jambo hilo limesababisha madalali kutwaa na kupiga mnada mali za watu na kuwaacha maskini. Kwa hivyo, tunajaribu kutetea kikundi hicho,” alisema Bw Wainaina.

Alisema mswada huo pia umeweka vikwazo kadha kwa wanaotaka kupewa zabuni kwa sababu kutakuwa na kutaka maelezo ya fedha wanazotarajia kulipwa kulingana na kazi ilivyofanywa, bila kuzidisha malipo zaidi.

“Tunajua mswada huo ukipitishwa rasmi bila shaka pande zote mbili zitakuwa na maelewano mwafaka kuhusu jinsi zabuni zitakavyotolewa,” alisema Bw Wainaina.

You can share this post!

Sofapaka yanasa saini za Roy Okal na Kevin Omondi

Polisi ashtakiwa kuiba vita vya Sh6 milioni