• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Sekta ya utalii kote duniani imepoteza zaidi ya Sh35 trilioni

Sekta ya utalii kote duniani imepoteza zaidi ya Sh35 trilioni

GENEVA, Uswisi

SEKTA ya utalii duniani imeathirika pakubwa kutokana na janga la virusi vya corona huku ikipoteza mabilioni ya hela kulingana na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Antonio Guterres.

Katibu huyo ameeleza kuwa sekta hiyo imepoteza zaidi ya Sh35 trilioni kutokana na bidhaa zinazouzwa katika mataifa ya kigeni huku ajira kwa watu zaidi ya 120 milioni ikiwa hatarini.

Kupitia kwenye hotuba kwa njia ya video, Guterres alisema idadi ya watalii ilipungua kwa zaidi ya nusu kwa sababu ya janga hilo la kiafya, ambalo limelemaza mifumo ya kiuchumi duniani.

“Utalii ndio sekta ya tatu kuu zaidi ulimwenguni baada ya mafuta na kemikali, huku ikitoa ajira kwa mtu mmoja miongoni mwa kila kundi la watu 10 kote duniani na asilimia 7 ya biashara ulimwenguni.”

“Ndiposa limekuwa jambo la kutamausha mno kuona jinsi utalii umesambaratishwa na janga la Covid-19,” alisema mkuu wa UN.

Janga la virusi vya corona limesababisha vifo vya watu zaidi ya 813,000 ulimwenguni kote huku kukiwa na visa zaidi ya 23.6 milioni, kulingana na data iliyokusanywa na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins.

Watu wapatao 15.3 milioni wamepata nafuu kufikia sasa.

Katika jaribio la kudhibiti kusambaa kwa virusi hivyo, mataifa kote duniani yamebuni mikakati thabiti ikiwemo kufunga shughuli nchini, kufunga viwanja vya ndege, kutangaza marufuku dhidi ya usafiri na kufunga mipaka yao kabisa.

Guterres alisema janga hilo limekuwa “tisho kuu” kwa mataifa tajiri yaliyoendelea lakini kwa “mataifa yanayoendelea, ni jambo la dharura, hasa kwa maeneo mengi ya visiwa na nchi za Kiafrika.”

Utalii kwa baaadhi ya mataifa unawakilisha zaidi ya asilimia 20 ya Kiwango cha Jumla cha Uzalishaji (GDP), kulingana na UN.

Mkuu wa Udadisi kuhusu soko na ushindani katika Shirika la Utalii Duniani, katika UN, Sandra Carvao, alisema Sh35 trilioni zilizopotezwa Januari hadi Mei, ni mara tatu zaidi ya kiasi kilichopotezwa mnamo 2009 katika kilele cha hali mbaya ya kifedha duniani.

Kulingana na taarifa za kisera, “mapato kutokana na utalii wa kuuza bidhaa katika mataifa ya kigeni huenda yakashuka kwa asilimia 1.5 hadi asilimia 2.8 ya GDP.”

You can share this post!

Ruto akutana na Lee Njiru

Mazishi ya dakika 20 ya aliyekuwa kinara wa...