• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
Mahabusu zaidi wahepa seli za polisi katika hali ya kutatanisha

Mahabusu zaidi wahepa seli za polisi katika hali ya kutatanisha

Na STEVE NJUGUNA

IDADI ya washukiwa wanaotoroka seli za polisi imeendelea kuongezeka huku 10 wakitoroka katika kituo cha polisi cha Ndaragwa, Kaunti ya Nyandarua mnamo Jumatatu usiku.

Polisi walisema washukiwa hao walitoroka kwa kukata vyuma vya dirisha mwendo wa saa nane za usiku. Wawili walikamatwa baadaye.

Habari zilisema kulikuwa na maafisa wanne wa polisi kazini wakati mahabusu hao walipohepa.

Afisa Mkuu wa polisi katika eneo la Nyandarua Kaskazini, Timon Odingo alisema washukiwa wengine watano waliachwa kwenye seli wenzao walipotoroka.

Polisi katika eneo hilo wamekuwa wakilalamika kutokana na idadi kubwa ya washukiwa wanaozuiliwa kwenye seli.

KAYOLE

Washukiwa wengine sita walitoroka kituo cha polisi cha Kayole mnamo Septemba 3.

Washukiwa hao waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka tofauti ikiwemo ujambazi na unajisi walitoroka kwa kukata vyuma vya madirisha.

Mnamo Agosti 16, washukiwa 11 walitoroka seli katika kituo cha polisi cha Bungoma kwa kutoboa shimo kwenye ukuta.

Polisi walisema kuwa walijulishwa na mahabusu wengine kuhusu kutoroka kwa wenzao mwendo wa saa tisa za usiku.

Mwezi Julai washukiwa wengine akiwemo raia wa Uingereza walitoroka katika hali tatanishi.

Visa hivyo vilitokea maeneo mbalimbali ya nchi, ambapo polisi walishindwa kueleza walivyotoroka.

Visa hivyo vilitokea katika kituo cha polisi cha Mtwapa (Kilifi), mahakama ya Kibera (Nairobi), vituo vya polisi vya Langas (Uasin Gishu), Nyamira na Naiberi (Uasin Gishu).

Wakuu wa polisi wamekuwa wakisita kueleza sababu ya ongezeko la visa vya mahabusu kuhepa.

You can share this post!

Wazee wa Kaya watisha kumlaani Jumwa kwa kumtetea Sudi

Watu 8 wauawa katika mapigano ya Legio Maria