• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
‘Mama ntilie’ mpishi kigogo wa kibandani

‘Mama ntilie’ mpishi kigogo wa kibandani

Na Ludovick Mbogholi

BI. Aisha Omar(40) anafanya kazi ya upishi katika eneo la Liwatoni, Ganjoni mkabala na eneo la viwanda na makampuni, na yeye ni mama anayetambuliwa sana kama ‘mama ntilie’. Mama huyu hajawahi kuingia darasani lakini kwa juhudi zake amepiga hatua kubwa kimaisha.

“Tangu nizaliwe sijaingia darasani kupata elimu na sijui masomo ni nini” apasha kwenye mahojiano yake na Akilimali.Bi. Aisha aliishi na wazazi huko Duga, Maforoni mkoani Tanga, Tanzania alikozaliwa.

“Kwa kuwa sina elimu, nilihisi afadhali nianze kujishughulisha na kazi ya upishi mitaani kwa kupika chapati, maharagwe, nyama, karanga, matumbo, githeri na muthokoi miongoni mwa vyakula vyengine” akariri Bi.

Aisha huku akidokeza kazi hiyo ndiyo iliyompatia jina la ‘mama ntilie’.Kazi ya upishi iliposhika kasi alitambuliwa zaidi na wateja huku umaarufu wake ukiwa kichocheo cha uamuzi wa kuhamisha shughuli zake katika eneo la Ganjoni huko Liwatoni kwenye watu wengi wanaofanya kazi viwandani na katika makampuni makubwa.

“Ilibidi nije hapa maana niliamini nitafanikiwa zaidi kimapato” akiri ‘mama ntilie’ huyu alipoendelea kuhojiwa na Akilimali kwenye eneo lake la kazi huku akisisitiza kusema kwa siku anatumia mifuko mitatu ya unga wa ngano kwa upishi wa chapati, na kila mfuko unampatia jumla ya chapati 28.

“Mfuko mmoja unanipatia chapati 28, na kila chapati nauza kwa Sh15” anadokezea Akilimali kwenye mahojiano huku ikiaminika anapata jumla ya chapati 84 kwa mifuko mitatu ya unga huo ambayo ni sawa na kilo 6 kwa jumla.Akilimali imebainisha kuwa kila siku Bi. Aisha huuza chapati 84 na kunufaika kwa Sh1,260.

Hata hivyo Bi. Aisha anasema anauza chapati hizo na maharagwe ambayo ndiyo mboga inayopendwa zaidi na wateja wake.

“Kila siku napika kilo mbili za maharagwe, na huwauzia wateja sahani moja kwa Sh30. Hii inamaanisha kuwa mteja akiagiza chapati mbili na maharagwe ananilipa Sh60” anaarifu zaidi kuhusu mapato anayojiingizia kwenye biashara yake hiyo.

Bi Aisha Omar hunufaika kwa pato la Sh2,760 kila siku kwani maharagwe pekee humwingizia takriban Sh1,500 kwa kilo mbili anazonunua kwa siku.Hata hivyo Akilimali imegundua kuwa ‘mama ntilie’ huyu hunufaika kwa takriban Sh82,800 kwa biashara ya chapati na maharagwe pekee kwa mwezi mbali na mauzo ya githeri, wali, muthokoi, ugali na chai miongoni mwa vyakula vingine anavyopikia wateja.Kwa jumla Bi.

Aisha Omar hujiingizia zaidi ya Sh100,000 kila mwezi, pato hilo huchangiwa na vyakula vingine vinavyomwingizia takriban Sh30,000 kila mwezi.“Hata hivyo nakumbana na changamoto nyingi zikiwemo kusumbuliwa na maafisa wa afya na wa kaunti” anapasha Akilimali huku akidai mafanikio hayo hayamtoshelezi maana kila siku anamlipa mfanyakazi wake Sh300 pesa taslimu.

Kwenye taarifa tofauti iliyogunduliwa na Akilimali, Bi. Aisha Omar amebahatika kufahamu zaidi ya lugha 20 za makabila tofauti yakiwemo ya Kimaasai, Kichagga, Kikuyu na Kisomali.

You can share this post!

Maseneta wamkaanga Oparanya kwa amri yake ya kufunga kaunti

Joto jingi Mandera lilivyo na tija kwa wakuzaji tikitimaji