• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Waziri mtatanishi

Waziri mtatanishi

Na MWANDISHI WETU

MISIMAMO ya Waziri wa Elimu, Prof George Magoha kuhusu ufunguzi wa shule tangu zilipofungwa Machi kwa sababu ya janga la corona, umewaacha wazazi, walimu na wanafunzi wamechanganyikiwa.

Tangu kisa cha kwanza cha maambukizi ya corona kutokea nchini na kusababisha shule zote kufungwa, Prof Magoha amekuwa katika mstari wa mbele kuarifu umma kuhusu hatua zinazochukuliwa na wizara yake.

Kila mara waziri huyo anapojitokeza kuhutubia umma, wadau wa elimu hasa wazazi na walimu husubiri kwa hamu kusikia wazi kuhusu ni lini shule zitakapofunguliwa.

Hata hivyo, mijadala ambayo hutokea miongoni mwa wadau wa elimu ikiwemo katika sehemu za umma na mitandao ya kijamii kila baada ya hotuba za Prof Magoha huonyesha huwa anawaacha wamekanganyika zaidi kila mara anapohutubu.

Mnamo Julai 1, Prof Magoha alitangaza kuwa uamuzi kuhusu kama shule zitafunguliwa ungetangazwa na Rais Uhuru Kenyatta mnamo Julai 6.

Wakati huo, alidokeza kuwa shule zitafunguliwa Januari mwaka ujao kwa vile wataalamu wa afya walisema maambukizi ya virusi vya corona yangefika kilele Septemba.

Awali, wizara hiyo ilikuwa imetangaza uwezekano wa shule kufunguliwa Septemba mwaka huu hasa kwa watahiniwa wa Darasa la Nane na Kidato cha Nne.

Wakati Rais Kenyatta alipohutubia taifa, hakuzungumzia suala hilo na badala yake akalirudisha mikononi mwa Prof Magoha ambaye alihutubu Julai 7.

“Wadau wameamua shule zitafunguliwa tu baada ya idadi ya maambukizi kupungua hadi chini ya asilimia tano ya wanaopimwa kwa wiki mbili mfululizo. Idadi ya maambukizi inapanda sana Kenya kwa sasa. Kwa kuzingatia haya, wadau wameamua kuachana na pendekezo la awali la kufungua shule Septemba,” alisema waziri.

Lakini baadaye mwishoni mwa Agosti, waziri alijitokeza tena na kudokeza uwezekano wa shule kufunguliwa karibuni, aliposema kamati maalumu inatazama hali itakavyokuwa kwa “wiki mbili au tatu zijazo”.

KAMATI MAALUM

Mapema wiki hii, uwezekano huu ulitiwa nguvu baada ya mkutano wa kamati maalumu ya wadau wanaotathmini hali ya elimu wakati wa Covid-19.

Ijapokuwa walikataa kutangaza kama wamekubaliana kufungua shule, Prof Magoha alisema utathmini umefanywa upya kwa vile idadi ya maambukizi ya virusi vya corona imekuwa chini mno kwa karibu wiki tatu sasa.

“Tumekubaliana kwa pamoja kwamba wakati umefika kufanya utathmini upya kwa sababu idadi ya maambukizi inapungua. Jinsi watoto watakavyokaa darasani bila kukaribiana ndiyo bado ni changamoto,” akasema.

Wanaomlaumu kwa kutapatapa wanasema Wizara ya Elimu inafaa kuwa na msimamo thabiti kuhusu mwelekeo ambao elimu inafaa kuchukua.

“Wizara muhimu kama hii ya Elimu ambayo hutegemewa na mamilioni ya Wakenya haifai kutapatapa. Tunahitaji msimamo thabiti kuhusu masuala yote. Lazima tuwaandae watoto wetu kisaikolojia kama watarudi shuleni Novemba au Januari,” Mwenyekiti wa kamati ya bunge kuhusu elimu, Bi Florence Mutua alisema wakati kulipokuwa na kikao mapema mwezi huu.

Hata hivyo, wadau wengine wamemtetea Prof Magoha na kusema misimamo yake huongozwa na ushauri kutoka kwa Wizara ya Afya kuhusu hali ya janga la corona ilivyo nchini.

Kulingana na Katibu Mkuu wa Chama cha Kitaifa cha Walimu (KNUT), Bw Wilson Sossion, serikali awali ilikuwa imetangaza shule zitafunguliwa Januari 2021 kwa sababu wataalamu wa afya walisema maambukizi yangefika kileleni kati ya Septemba na Oktoba.

You can share this post!

WANDERI: Tofauti za kidini zafaa zitatuliwe kwa utulivu

Wakufunzi wapya wa Kabras RFC kutua nchini Jumamosi