• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
Wamiliki wa baa wasema ‘wamesota’, hawana hela za kurejelea biashara

Wamiliki wa baa wasema ‘wamesota’, hawana hela za kurejelea biashara

Na SAMMY WAWERU

Matamshi ya Rais Uhuru Kenyatta “sasa mnaweza kunywa pombe” yakiashiria kuruhusu ufunguzi wa mabaa, vilabu na maeneo ya burudani miezi sita baada ya kufungwa kama kati ya mikakati iliyotolewa kuzuia msambao wa Covid-19, yalikaribishwa na wengi hasa waraibu wa vileo.

Baada ya kiongozi wa nchi kutoa tangazo hilo mnamo Jumatatu, baadhi ya waraibu wa pombe walizua utani wakihoji, “Jumanne tutaamkia kuwa wageni wa mabaa”.

Huku kauli ya Rais Kenyatta ikiwa afueni kwa wamiliki wa mabaa na wapenzi wa pombe, baadhi yao wanasema hawana pesa kufufua biashara zao kutokana na athari za Homa ya virusi vya corona.

Margaret Wanjiku ni mmoja wa wafanyabiashara wa vileo Nairobi na ameiambia Taifa Leo kwamba baada ya amri ya mabaa, vileo na maeneo ya burudani kufungwa kutolewa, kipindi kilichofuata amekuwa akitumia fedha alizoweka kama akiba kukithi familia yake riziki.

Kulingana na Wanjiku, pia amekuwa akifanya vibarua vya hapa pale ili kukimu familia yake mahitaji muhimu ya kimsingi. “Ndio, tunafurahia tangazo la Rais mabaa yafunguliwe, ila kwa sasa hatuna pesa kuifufua,” akasema, akieleza kwamba chumba lilipokuwa baa lake alikuwa akikodi.

“Singeendelea kulipia kodi ilhali uuzaji wa pombe ulikuwa marufuku. Nililazimika kurejesha vifaa kwenye nyumba, nikisubiri uchumi ufunguliwe tena. Ukweli ni kwamba sina uwezo kufufua biashara yangu,” akasema mama huyo wa watoto wawili, akiomba serikali ipige jeki wafanyabiashara wa pombe.

Aidha, Rais Kenyatta amewataka wafanyabiashara wa vileo pindi watakapofungua mabaa na vilabu, watii sheria na mikakati iliyowekwa kuzuia kusambaa kwa corona.

“Kuanzisha biashara ya pombe iliyoafikia leseni na mahitaji yote si rahisi. Si ajabu mmiliki akitumia zaidi ya Sh500, 000 kuimarisha baa la kadri,” akadokeza mmiliki mwingine mtaa wa Githurai, ambaye alisema yuko katika harakati za kutafuta hela kurejea katika biashara ya pombe.

Kufuatia athari za corona kwa biashara na uchumi kuyumbishwa, kwenye uchunguzi wa Taifa Leo imedhihirika baadhi ya wamiliki wa mabaa na vilabu wamelazimika kukodi maeneo waliyotumia, kwa wenye uwezo kifedha kuwekeza katika biashara ya pombe.

Katika eneo la Mirema, mtaa wa Zimmerman, Nairobi, mmoja wa wamiliki wa vilabu ameweka notisi ya kukodisha kilabu chake na juhudi za kumfikia kwa njia ya simu kupitia nambari alizoweka hazikufua dafu, kwani ilikuwa imezimwa hadi wakati wa kuchapisha taarifa hii.

Kuna mabaa yaliyosalia kufungwa licha ya Rais kuyaruhusu kuhudumu. Aidha, mengine yamegeuzwa maduka ya bidhaa za kula.

Wenye maduka ya kuuza vileo vya kubebwa (take away), ndio wamekuwa wakihudumu chini ya kanuni walizowekewa na Wizara ya Afya.

You can share this post!

Wito serikali idhibiti maajenti wanaowapeleka Wakenya...

Niko tayari kwa EACC kunipiga darubini – Joho