• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 11:13 AM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Nguzo tano za Uislamu ni mfumo wa maisha ya kawaida kwa Muumini

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Nguzo tano za Uislamu ni mfumo wa maisha ya kawaida kwa Muumini

Na HAWA ALI

SIFA zote njema anastahiki Mungu Azzawajalla, swala na salamu zimwendee Mtume Mtukufu Swallallahu A’alayhi Wasallam.

Nguzo tano za Uislamu ni mfumo wa maisha ya Mwislamu. Ndizo ushahidi wa Imani, Swalah, utoaji wa Zakaah (kuwasaidia wenye dhiki), kufunga katika mwezi wa Ramadhan na kuhiji Makkah mara moja maishani kwa wale wenye uwezo.

1 Shahada ya Imani

Ushahidi wa Imani ni kusema kwa kusadikisha, “La ilaaha illAllaah, Muhammadur Rasulullah.” Maana ya matamshi haya ni, “Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu (Allaah), na kwamba Muhammad ni Mjumbe (Mtume) wa Mwenyezi Mungu.” Sehemu ya kwanza, “Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki, isipokuwa Mwenyezi Mungu,” inamaanisha kwamba hapana mwenye haki ya kuabudiwa isipokuwa Mwenyezi Mungu peke yake, na kwamba yeye hana mshirika wala mwana.

Ushahidi huu wa Imani unaitwa Shahada, ambayo ni kanuni nyepesi inayopaswa itamkwe pamoja na kusadiki ili mtu aweze kuingia katika Uislamu, kama ilivyoelezwa hapo juu. Ushahidi wa Imani ndiyo nguzo muhimu zaidi katika Uislamu.

2 Swalah

Waislamu huswali Swalah tano kila siku. Kila Swalah huchukuwa muda mfupi wa dakika chache tu. Swalah katika Uislamu ni mawasiliano ya moja kwa moja kati ya mja na Mwenyezi Mungu. Hakuna kishenga baina ya Mwenyezi Mungu na mfanyaja ibada.

Ndani ya Swalah, mtu husikia ndani yake furaha, amani na faraja, na kwamba Allaah yu radhi naye. Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: (Bilaal adhini, ili tufarijike nayo.)

Bilaal alikuwa mmojawapo wa Maswahaba wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na alikuwa mwadhini. Swalah hufanyika wakati wa Alfajiri, Adhuhuri, Alasiri, Magharibi na ‘Ishaa. Mwislamu anaweza kuswali karibu pahala popote, kama vile mashambani, ofisini, viwandani au vyuoni.

3 Kutoa Zakaah

Kila kitu ni cha Mwenyezi Mungu, na hata mali zinazohifadhiwa na wanadamu kama dhamana. Maana halisi ya neno Zakaah ni zote mbili ‘kutwaharisha’ na ‘kukua.’ Maana ya kutoa Zakaah ni kutoa asilimia iliyotajwa bayana kutokana na mali fulani kwa kuwapatia makundi fulani ya watu wenye dhiki.

Asilimia inayopaswa kulipwa kutokana na dhahabu, fedha na pesa taslimu zenye kufikia kiasi kinacholingana na gramu 85 za dhahabu na kubaki katika miliki ya mtu kwa mwaka mmoja wa Kiislamu ni asilimia mbili na nusu. Tunavyovimiliki hutakasika kwa kutenga pembeni sehemu ndogo tu kwa ajili ya wenye dhiki, na kama vile kupogoa matawi ya mimea, huku kupunguza salio na kunatia moyo wa ukuaji mpya. Mtu anaweza kutoa zaidi kadri atakavyo kama Sadaka.

4 Kufunga katika Mwezi wa Ramadhan

Kila mwaka katika mwezi wa Ramadhan, Waislamu hufunga kuanzia alfajiri hadi kuchwa kwa jua, kwa kujizuia kula, kunywa na tendo la ndoa. Ingawa Swawm ni yenye faida za kiafya, huchukuliwa kimsingi kuwa ni namna ya kuisafisha nafsi kiroho.

Kwa kujizuia dhidi ya starehe za kidunia, japo kwa muda mfupi, mfungaji hupata huruma ya kweli kwa wanaopatwa na njaa, kadhalika na kuongezeka kwa maisha yake ya kiroho.

5 Kuhiji Makkah

Hija ya kila mwaka Makkah ni faradhi ya kufanywa mara moja tu maishani kwa wenye uwezo wa kimwili na mali katika kuitekeleza. Kadri ya watu milioni mbili huenda Makkah kila mwaka kutoka kila sehemu duniani. Ingawa mara zote Makkah huwa imesheheni wageni, Hija ya mwaka hufanywa katika mwezi wa kumi na mbili katika kalenda ya kiislamu. Mahaji wa kiume huvaa nguo maalumu na rahisi ambayo huondosha tofauti za kimatabaka na tamaduni kiasi kwamba wote huwa sawa mbele ya Mwenyezi Mungu.

Mahujaji wakiswali katika Msikiti wa Haram huko Makkah. Msikitini humu mna Ka’abah (jengo jeusi linaloonekana katika picha) ambalo Waislamu hulielekea wakati wakiwa katika Swalah. Ka’abah ni mahali pa ibada ambapo Mwenyezi Mungu Aliwaamuru Mitume Ibraahiym na mwanaye, Isma’iyl waijenge.

Ibada za hija ni pamoja na kuitufu Ka’abah mara saba na kwenda mchakamchaka baina ya kilima cha Swafa na Marwa mara saba, sawa na Hajar alivyofanya wakati akitafuta maji. Kisha, Mahujaji husimama pamoja katika uwanja wa ‘Arafah na kumwomba Mwenyezi Mungu wakipendacho na kwa ajili ya maghufira, katika kile ambacho mara nyingi hufikirika kuwa ni onyesho la awali la Siku ya Malipo.

Mwisho wa Hijjah huweza kujulikana kwa sikukuu ya ‘Iydul-Adhw-haa, ambayo husherehekewa kwa Swalah. Sikukuu hii na ‘Iydul-Fitwr, sherehe ya kuadhimisha mwisho wa Ramadhan ndiyo sikukuu mbili za kila mwaka katika kalenda ya Kiislamu.

You can share this post!

Huenda Kenya ikose Jaji Mkuu kwa miezi 6

Ubunge kuokoa vigogo kisiasa