• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 9:58 AM
TAHARIRI: Mgomo wa maafisa wa afya utaleta maafa Krismasi

TAHARIRI: Mgomo wa maafisa wa afya utaleta maafa Krismasi

NA MHARIRI

IKIWA madaktari wataanza mgomo wao Jumatatu hii walivyotangaza, kuna hatari ya maafa makubwa kutokea Kenya wakati huu wa likizo ya Krismasi.

Hii ni kwa sababu sekta ya afya italemazwa kabisa kwa kuwa wahudumu wengine wa afya wanaendelea kugoma.

Madaktari wanagoma wiki mbili baada ya wauguzi na matibabu kugoma kumaanisha kuanzia leo hakutakuwa na huduma zozote katika hospitali za umma.

Kuna uwezekano hali hii huenda ikadumu kwa muda kufuatia kauli ya waziri wa afya Mutahi Kagwe kwamba wahudumu wote wa afya wanaogoma wanafaa kufutwa kazi na wengine kuajiriwa kuchukua nafasi zao.

Bila shaka, hii haitakuwa tiba kwa mzozo unaokumba sekta ya afya kwa sababu watakaoajiriwa, watajipata katika hali sawa na watangulizi wao na hali kujirudia.

Hii inavyofanyika, na ndivyo inavyotarajiwa, masikini wanaotegemea hospitali za umma kwa matibabu watakuwa katika hatari kubwa hasa wale wanaoambukizwa virusi vya corona.

Inasikitisha wanasiasa na maafisa wa serikali, baadhi yao madaktari waliohitimu, wanaweza kupuuza maslahi ya Wakenya wanaolipa ushuru wanaofurahia wanapoenda kutibiwa katika hospitali za kibinafsi ambao wengi hawawezi kumudu.

Inasikitisha badala ya kutoa mwelekeo unaoweza kupunguzia wagonjwa mateso, maafisa wa serikali wanatisha kuwafuta kazi. Kuna haja ya kutatua mzozo huu kwa njia ya mazungumzo na hii haiwezi kuafikiwa kupitia vitisho na misimamo mikali.

Maafisa wa serikali wanaelewa kwamba madaktari wameambukizwa corona na kufariki wakiwa kazini. Hawa ni wale ambao maafisa wa serikali walikuwa wakiwamiminia sifa na kuahidi kuwasaidia kukabiliana na virusi vya corona.

Je, ni nini kiligeuka ikafikia kutoka vitisho wahudumu wa afya wanapotaka wapatiwe vifaa bora vya kazi kuwakinga dhidi ya maambukizi wakiwa kazini?

Je, kuna njama ya kusababisha vifo vya halaiki kwa sababu ya Wakenya kukosa huduma za afya?

Serikali inataka Wakenya wangapi wakiwemo madaktari wafariki ili isikie kilio cha wahudumu wa afya? Kabla ya maswali haya kupata majibu huenda maafa makubwa yakatokea Kenya kwa sababu ya suala ambalo linahitaji nia njema kutatua.

 

You can share this post!

Usasa ulivyoyeyusha utamaduni wa Ameru

CECIL ODONGO: Raila na Ruto wasiamulie wananchi viongozi wao