• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 2:55 PM
Hatuwezi kutazama mamilioni ya mafuta yakifyonzwa KPC – Halakhe Waqo

Hatuwezi kutazama mamilioni ya mafuta yakifyonzwa KPC – Halakhe Waqo

Na CHARLES WASONGA

Afisa Mkuu Mtendaji wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) Halakhe Waqo Jumanne alitofautiana vikali na wabunge kuhusu sakata ya Sh660 milioni katika Kampuni ya Mafuta Nchini (KPC).

Huku wanachama wa Kamati ya Bunge kuhusu Kawi wakidai sio makosa kwa kampuni za humu nchini kuwa maajenti wa kampuni za ng’ambo kuhusiana na suala la utoaji wa zabuni, wanachama wa kamati hiyo walishikilia hiyo sio makosa.

Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo Robert Pukose na mbunge wa Butere Tindi Mwale walidai haikuwa kosa kwa kampuni ya Cla-Val kuiuzia KPC mitambo ya kujaza mafuta kwa ndege (Hydrant Pit Valve-HPV) kwa bei ya juu, Bw Waqo alisema hatua hiyo ni kinyume cha sheria za ununuzi bidhaa za umma.

“Sioni makosa yoyote kwa kampuni ya Cla-Val kutumia kampuni ya Aero Dispenser Valve kama ajenti wake wa kuuza mitambo kama hii, hata kama itakuwa kwa bei ya juu,” akasema Dkt Pukose ambaey ni Mbunge wa Endebess.

Lakini Bw Waqo alishikilia kuwa ilikuwa hatua ya wizi wa waziwazi kwa kampuni ya Aero Dispenser kununua mitambo hiyo kwa Sh72 milioni kutoka kwa Cla-Val kisha kuiuzia KPC kwa bei ya Sh660 milioni, hivyo kuunda faida ya zaidi ya asilimia 800.

“Huu ni wizi ya pesa za umma na sisi katika EACC hatutakaa kitako uovu kama huu ukiendelea,” akasema Afisa huyo alipofika mbele ya kamati hiyo kuelezea hatua ambayo EACC imepiga katika uchunguzi wa kashfa hiyo.

Bw Waqo aliwaambia wabunge hao kwamba tume yake itapendekeza kushtakiwa kwa wahusika wote wa kashfa hiyo ambayo imewaweka pabaya baadhi ya maafisa wa KPC.

Katika sakata hiyo maafisa wa KPC walipeana zabuni ya Sh660 milioni kwa ununuzi wa mitambo ya kujaza mafuta kwa ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa (JKIA) badala ya Sh59 milioni, bei halisi kutoka kampuni ya Cla-Val kutoka Amerika.

Afisa mkuu mtendaji wa tume hiyo Halakhe Waqo jana aliwaambia wabunge kuwa watawasilisha faili ya uchunguzi huo kwa afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Noordin Haji ili washukiwa hao washtakiwe kwa wizi wa pesa za umma.

“Tumepata usaidizi kutoka mataifa ya Amerika na Canada katika uchunguzi wetu na sasa tuko ya ushahidi tosha kuhimili kesi mahakama. Mapema wiki ujao tutawasilisha faili yenye ushahidi tosha kwa DPP,” Bw Waqo akasema alipofika mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Kawi, katika majengo ya bunge.

Afisa huyo aliwaambia wanachama cha kamati hiyo kwamba japo KPC ilipaswa kununua mitambo hiyo kwa Sh59 milioni maafisa wake walishirikiana na kampuni za Aero Dispenser Valve Ltd kukubali bei ya Sh660 milioni.

“Na mnamo Machi 31, 2015 kampuni hiyo ambayo tumebaini ni feki ililipwa malipo ya awali ya Sh262 milioni, kiasi sawa na asilimia 40 ya thamani ya zabuni hiyo huku zilisalia Sh400 milioni” akasema.

Akauliza: “Swali letu ni je, ni nani aliamuru kwamba biashara hiyo ipewe kampuni ya Aero Dispenser Valve ilhali kamati ya zabuni ya KPC ilipendekeza ipewe watengenezaji hali ya mitambo hiyo ambayo ni kampuni ya Cla-Val ya Amerika?.

Bw Waqo alisema japo uchunguzi wao umedumu kwa zaidi ya miaka mitatu hatimaye EACC imebaini ukweli kwamba wafanyakazi wa KPC walishiriki njama ya kuiba pesa za umma kwa kupandisha bei ya mitambo hiyo kupita kiasi.

You can share this post!

Waiguru atisha kumshtaki Jicho Pevu kwa kumhusisha na wizi...

Likizo ya lazima kwa wakuu wa NCPB

adminleo