• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
PEPO WA MIGOMO: Shule 30 zafungwa, wanafunzi wachoma mali ya mamilioni

PEPO WA MIGOMO: Shule 30 zafungwa, wanafunzi wachoma mali ya mamilioni

Na WAANDISHI WETU

PEPO ya migomo imeitembelea tena Kenya huku Waziri wa Elimu Amina Mohamed akitaja hofu ya mitihani kama kiini kikuu cha fujo zinazoshuhudiwa shule nyingi hasa za sekondari.

Katika miaka ya majuzi imekuwa jambo la kawaida kwa migomo na uharibifu wa mali katika shule za sekondari kushuhudiwa.

Waziri Mohamed alisema hayo huku shule zaidi ya 30 zikiathiriwa na migomo na mabweni kuchomwa.

Shule hizo ni pamoja na Maranda High, Kisumu Girls, Ng’iya, Ambira, Maliera, Onjiko, Otieno Oyoo, Chulaimbo, Oriwo, Ngere, Kandiege, Usenge, Barding, St Augustine Nyamonye, St Marys Girls, Mumias na Litein Boys.

Pia kuna Kitondo, Nduluku Good Shepherd Girls, Kikuumini, Kyeemundu kutoka Mashariki. Zingine ni Kathera Boys, Thuura, Mukuiru, Kisima, St Lukes na Meru.

Katika visa vya majuzi vya migomo hiyo, wanafunzi 30 wa shule ya kibinafsi ya Kenyenya katika Kaunti ya Kisii walikesha kwenye baridi usiku wa kuamkia jana baada ya shule hiyo kukumbwa na moto.

Kwa mujibu wa wanafunzi, bweni moja liliteketea wakati wanafunzi walipokuwa madarasani kwa masomo ya ziada.

Nayo shule ya Upili ya Wavulana ya Chewoyet, Kaunti ya Pokot Magharibi ilifungwa kwa muda usiojulikana baada ya bweni moja kuchomeka jana asubuhi.

Mali yenye thamani isiyojulikana iliteketea katika bweni la Longonot ambalo huwa na wanafunzi 115.

OCPD wa Kapenguria Bw Anthony Wanjuu alisema moto huo ulianza majira ya saa kumi na moja alfajiri wakati wanafunzi walipokuwa kwenye masomo ya ziada .

Katika juhudi za kukabiliana na migomo hiyo, alisema Bi Mohamed, wanafunzi watatu wa shule ya Siakago High iliyoko Kaunti ya Embu wamefungwa jela kwa mwaka mmoja huku wanafunzi 125 wa shule mbalimbali wakikamatwa kuhusiana na migomo inayoendelea.

Haya yanajiri wakati Idara ya Upelelezi (DCI) imetangaza kukusanya habari kuhusu wanafunzi wanaochochea migomo na kujaribu mali kwa lengo la kuweka rekodi ambazo zitatumiwa wakati wa maombo ya Vyeti vya Tabia Njema wanapomaliza masomo. Vyeti hivyo huhitajika na waajiri wengi.

Bi Mohamed alisema mikakati iliyowekwa kuzuia udanganyifu katika mitihani ya kitaifa imechangia pakubwa migomo hiyo. Pia ameeleza kuwa ukosefu wa nidhamu kwa jumla unachangia matukio hayo.

Waziri alieleza kuwa ripoti ya mapema ya wizara imeonyesha hilo huku akitoa mfano wa tukio katika shule ya Chalbi, Marsabit ambapo wanafunzi waliwavamia walimu ambao si wenyeji.

“Wanafunzi hao pia walimtaka mkuu wa shule kuwahakikishia kuwa watasaidia wizi wa mitihani,” alieleza, akisema jambo hilo linastahili kumtia hofu kila mmoja.

“Hii ndiyo sababu nitasafiri Nyanza kubaini chanzo cha baadhi ya shule ambazo hazijawahi kushuhudia fujo kuwa na hali hiyo sasa. Ninataka kujua ni nini kilifanyika na nini kilichochea. Ikiwa ni mitihani, basi ieleweke kuwa sote lazima tufanye bidii kupita mitihani yetu,” alisema.

Alieleza kuwa wizara inaunga mkono hatua ambazo zimechukuliwa na idara ya upelelezi nchini kuwa wanafunzi wanaojihusisha na migomo shuleni watakabiliwa na mashtaka ya uhalifu.

“Hii ni kuonya kila mwanafunzi kuanzia shule ya msingi, sekondari, vyuo vya kadri na vikuu kuwa DCI inaweka maeleo ya kila tukio la uhalifu na kuunganisha mashtaka ambayo huenda yakapendekezwa kwa kila mwanafunzi anayehusika na uhalifu,” idara hiyo ilieleza.

Idara hiyo ilieleza kuwa matukio hayo yatawaathiri wakifuta vyeti vya nidhamu njema, mbali na kuwa rekodi ya uhalifu itadumu katika maisha yao na huenda ikawazuia hata wanapotafuta ajira.

LUCY KILALO, JADSON MANDUKU NA OSCAR KAKAI

You can share this post!

Magavana waomba wasikamatwe kwa ufisadi

Mwafaka uliua nguvu za NASA, asema Mudavadi

adminleo