• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:07 PM
ICC yafikisha miaka 20 huku ikikosolewa

ICC yafikisha miaka 20 huku ikikosolewa

Na VALENTINE OBARA

MAHAKAMA ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) Jumatatu itaanza maadhimisho ya miaka 20 tangu ilipobuniwa Julai 17, 1998 huku makali yake ya kutenda haki kuhusu dhuluma za kivita kimataifa yakizidi kutiliwa shaka.

Viongozi wa Afrika bado wanalalamika kuhusu ICC ambayo wanadai hutumiwa kuingilia uhuru wa bara hili ikizingatiwa kuwa karibu kesi zote zilizo mbele yake ni za mataifa ya Afrika.

Mkataba wa Roma, ambao ndio msingi wa sheria za ICC, uliundwa katika mwaka wa 1998 na kuidhinishwa na mataifa 123 kufikia sasa, mengi yakiwa ni ya Afrika.

“Kuundwa kwa Mkataba wa Roma katika mwaka wa 1998 ilikuwa ni tukio la kihistoria na hatua kubwa katika juhudi za kutenda haki ulimwenguni. ICC inaazimia kupata ushirikiano kimataifa kulinda kila mtu kutokana na aina za uhalifu zilizotajwa kwenye Mkataba wa Roma,” mahakama hiyo ilisema kwenye taarifa.

Aina za uhalifu ambazo hupelekwa katika mahakama hiyo ni kuhusu uhalifu wa kivita ikiwemo mauaji ya halaiki, utumizi wa watoto katika vita na ubakaji wakati wa vita.

Muungano wa Afrika (AU) ulipinga zaidi mahakama hiyo wakati wa kesi zilizowakumba Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto kuhusiana na ghasia za baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2007.

Ingawa kesi hizo zilizojumuisha Wakenya wengine wanne zilianza 2010 kabla wawili hao waingie mamlakani mwaka wa 2013, AU ilighadhabishwa na jinsi walivyohitajika kuwa kizimbani licha ya kuwa viongozi wa taifa lililo huru.

Kesi zote zilisitishwa baada ya upande wa mashtaka unaoongozwa na Bi Fatou Bensouda kusema hapakuwa na ushahidi wa kutosha kuhukumu washukiwa.

“Nimekuwa nikisema mahakama itakuwa ya kushtaki Waafrika pekee, na sidhani kama nimekosolewa. Kuna watu wengi ulimwenguni ambao wanafaa kushtakiwa na mahakama hiyo,” Rais wa Rwanda, Paul Kagame ambaye pia ni Mwenyekiti wa AU alisema hivi majuzi.

Kwa sasa, viongozi barani wanamtetea Rais wa Sudan Omar al-Bashir ambaye kuna agizo la kukamatwa kwake lililotolewa na ICC.

Rais huyo huzuru mataifa mbalimbali ya Afrika ambapo viongozi wa Au wamekubaliana kutotekeleza agizo la kumkamata na kumfikisha ICC.

You can share this post!

Mbunge na mumewe watimuliwa gesti kwa kukosa cheti cha ndoa

Wataalamu nao waunga mkono Katiba igeuzwe

adminleo