• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Bidhaa ghushi za Sh7.5 bilioni zimenaswa, walaghai 75 wamezimwa – Ripoti

Bidhaa ghushi za Sh7.5 bilioni zimenaswa, walaghai 75 wamezimwa – Ripoti

NA CECIL ODONGO

MISAKO ambayo imekuwa ikiendeshwa na serikali dhidi ya bidhaa ghushi nchini tangu Juni 2018 imenasa bidhaa zenye thamani ya Sh7.5 bilioni, serikali ilisema Jumanne.

Operesheni hiyo pia imewanasa walaghai 75 miongoni mwao maafisa 10 wa serikali ambao tayari wamekamatwa na kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya ufisadi.

Katika taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya habari, Naibu Mkuu wa utumishi wa umma Wanyama Musiambo alisema kwamba thamani ya sukari ghushi ndiyo  ilikuwa  juu zaidi  kushinda bidhaa nyingine zilizonaswa.

“Kati ya Sh 7.5 bilioni, thamani ya sukari ghushi ilikuwa  Sh5.3 bilioni. Bidhaa za sigara (Sh828milioni), kilimo(Sh341milioni), vifaa vya stima(Sh300milioni), na pombe(Sh241milioni) pia zilichangia thamani hiyo,” ikasema taarifa ya Bw Musiambo.

Serikali pia imezamia mbinu kabambe ya kuhakikisha bidhaa ghushi haziingizwi nchini kwa kuimarisha ukaguzi na usalama kwenye miji ya mipaka. Mipaka iliyotajwa ni Busia, Malaba, Isbania, Shimoni, Moyale, Lunga Lunga na bandari ya Mombasa.

Hata hivyo maafisa waliojukumiwa kuhakikisha bidhaa haziingizwi nchini kiharamu watakuwa na beji maalum kama kitambulisho chao kitakachowatofautisha na wakora wanaojifanya maafisa halali kwa lengo la kuwapunja wafanyabiashara wanaotumia njia za kisheria kuingiza bidhaa nchini.

“Maafisa wanaoendesha misako hii wanatoa onyo kwa umma kujihadhari na wahalifu wanaojifanya kuwa maafisa halali ingawa lengo lao ni kulaghai wafanyabiashara. Maafisa wetu wana beji maalum na hufuata sheria bila kuwahangaisha wafanyabiashara, kuvunja maduka yao au kufunga biashara halali,” ikasisitiza taarifa hiyo.

Afisa huyo wa serikali alifichua kwamba bidhaa zote ghushi zilizonaswa zitaharabiwa huku juhudi zote zikifanywa kuhakikisha mtandao wa kuagiza na kusambaza bidhaa ghushi unaomilikiwa na wafanyabiashara wakora unaangamizwa.

Aidha aliwataka wananchi kuungana na serikali kufaulisha vita dhidi ya bidhaa ghushi kwa kuwa ni moja ya changamoto zinazotatiza kutimizwa kwa nguzo nne za utawala wa Rais Uhuru Kenyatta ikiwemo nguzo muhimu ya uundaji bidhaa.

You can share this post!

Kerr mwingi wa shukrani kwa kikosi baada ya kuibuka kocha...

Kesi dhidi ya waziri wa kaunti aliyeaga yatupwa

adminleo