• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
ONYANGO: Raila atumie ukuruba na Uhuru kuleta mageuzi

ONYANGO: Raila atumie ukuruba na Uhuru kuleta mageuzi

Na LEONARD ONYANGO

KIONGOZI wa Wengi Bungeni Aden Duale amegonga ndipo kwa kuhimiza Rais Uhuru Kenyatta na kinara wa ODM Raila Odinga kutekeleza ripoti ya Tume ya Ukweli, Haki na Maridhiano (TJRC).

Wito huo wa Bw Duale umeshutumiwa vikali na wakosoaji wake kwa sababu amekuwa miongoni mwa viongozi wa ngazi za juu wa Jubilee ambao wamekuwa wakipinga kutekelezwa kwa ripoti ya TJRC kutokana na kigezo kwamba itatonesha vidonda vya zamani.

Hata hivyo, wito huo wa Bw Duale unastahili kukumbatiwa na wanasiasa wote kutoka Jubilee na mrengo wa Upinzani; kuhakikisha kuwa ripoti hiyo ambayo imetelekezwa tangu 2013 inatekelezwa kikamilifu.

Rais Kenyatta alipokuwa akihutubia bunge la kitaifa mnamo 2015, aliomba msamaha kwa dhuluma zilizotekelezwa na serikali za marais waliomtangulia.

Katika hotuba yake kwa taifa mnamo 2017, Rais Kenyatta aliagiza Bunge kujadili ripoti hiyo. Lakini baadaye chama cha Jubilee kiligeuka na kusema kuwa utekelezwaji wa ripoti hiyo utazua uhasama dhidi ya baadhi ya jamii.

Kutekelezwa kwa ripoti ya TJRC ni miongoni mwa ajenda kuu ambazo Bw Odinga aliahidi kutekeleza endapo angefanikiwa kuingia Ikulu katika uchaguzi wa Agosti 8, mwaka jana.

Bw Odinga pia aliahidi kutoa elimu ya bure kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, kurejeshwa kwa maziwa kwa wanafunzi, kupunguzwa kwa kodi ya nyumba, kuwapunguzia wananchi gharama ya maisha, kuhakikisha wazee wanapata msaada wa fedha kila mwezi kati ya ahadi nyinginezo.

Wiki iliyopita, Bw Odinga katika mahojiano na runinga moja ya humu nchini alifichua kuwa siku hizi anakemea na kuripoti sakata za ufisadi kwa kumpigia simu Rais Kenyatta.

Bw Odinga alisema tangu kutia saini mwafaka wa ushirikiano na Rais Kenyatta amesitisha mbinu yake ya zamani ambapo aliita wanahabari kufichua sakata ya ufisadi na badala yake anampigia simu Rais Kenyatta moja kwa moja.

Ni kweli kwamba Rais Kenyatta ameorodhesha miradi yake mikuu minne; ujenzi wa nyumba nafuu, matibabu bora ya gharama ya chini, uboreshaji wa viwanda na uzalishaji wa chakula cha kutosha, anayopanga kushughulikia kabla ya kustaafu 2022.

Lakini, Bw Odinga anaweza kutumia ukuruba wake na Bw Odinga kushinikiza kutekelezwa baadhi ya ahadi alizotoa mwaka jana kama vile kutekelezwa kwa ripoti ya TJRC, elimu ya bure kutoka shule za msingi hadi sekondari, kupunguza kodi ya nyumba kati ya ahadi nyinginezo.

Baadhi ya ahadi zilizotolewa na Bw Odinga zinaingiliana na miradi minne mikuu inayoshughulikiuwa na Rais Kenyatta.

Kwa mfano, kupunguza kodi ya nyumba inaingiliana na mradi wa Rais Kenyatta wa kutaka kujenga nyumba za bei nafuu.

You can share this post!

TAHARIRI: Tunawapa wabunge alama ya ‘E’ kwa...

Polo atimuliwa na mahari yake ya kuku

adminleo