Habari

Amuua mpwa wake ili ajitajirishe na mamilioni ya bima

August 15th, 2018 1 min read

NA PETER MBURU

MWANAMUME anayetuhumiwa kumuua mpwa yake ili kudai Sh9 milioni kutoka kwa kampuni za bima hatimaye amefikishwa kortini na kufunguliwa mashtaka ya mauaji.

Mshukiwa, Evans Masaku Kasyoki alifikishwa katika mahakama za Kangundo Jumatano, ambako amri ilitolewa apelekwe katika hospitali ya Mathare jijini Nairobi kwanza kupimwa ikiwa yuko timamu.

Mshukiwa atazuiliwa katika jela ya Machakos GK hadi Septemba 17 wakati kesi yake itatajwa, baada ya kunyimwa bondi.

Kushikwa kwake kulijia mwaka mmoja baada ya kisa chake kuchukua bima mbili za maisha kwa mpwa wake ambaye hakuwa na chochote, kupanga mauaji yake na kisha maiti ya marehemu kutupwa eneo la Kangundo kumulikwa.

Baada ya mauaji hayo, mshukiwa anadaiwa kuharakisha kuzidai kampuni za bima malipo.

Mshukiwa, ambaye alikuwa mfanyakazi katika kampuni ya bima alikuwa amemchukulia bima ya Sh10 milioni na Sh1 milioni mpwa wake wa miaka 27 kutoka kwa kampuni mbili tofauti.

Hata hivyo, mauaji ya marehemu yalitokea mwezi mmoja tu baada ya mshukiwa kuanza kulipia bima.

Mnamo Jumapili, runinga ya Citizen ilieleza namna utepetevu miongoni mwa maafisa wa polisi ulisababisha mshukiwa kuachiliwa huru hata baada ya kukamatwa, huku wazazi wa marehemu wakiishi kwa kilio.