Dimba

Muyoti aapa Nai Boys’ wataonyesha Gor kivumbi fainali ya Mozzart Bet

Na CECIL ODONGO June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KOCHA wa Nairobi United Nicholas Muyoti ameeleza imani yake kuwa wataandikisha historia na kuwaangusha Gor Mahia kwenye fainali ya Kombe la Mozzart Bet mnamo Jumapili.

Mshindi wa mechi hiyo atafuzu Kombe la Mashirikisho Afrika (Caf) msimu ujao wa 2025/26.

Timu hizo mbili zitapepetana kwenye mechi kali ya fainali uga wa Ulinzi Sports Complex, Nairobi kuanzia saa 10 mchana.

Mshindi ataenda nyumbani na jumla ya Sh2 milioni huku nambari mbili akipokezwa Sh1 milioni.

Pia kutakuwa na mechi ya kusaka mshindi wa tatu ambapo Murangá Seal itavaana na Mara Sugar kuanzia saa sita mchana.

Mshindi wa nafasi ya tatu naye atapokezwa Sh750,000 huku nambari nne akipata Sh500,000 kutoka kwa wadhamini wa kombe hilo Mozzart Bet.

Nairobi United itakuwa ikilenga kushiriki Caf kwa mara ya kwanza huku Gor ikilenga kufuta machozi ya kukosa Ligi Kuu (KPL) kwa kushinda Mozzart Bet.

“Historia haitaisaidia Gor Mahia kwa sababu itakuwa wachezaji 11 dhidi ya 11 na hii ni fainali waelewe kuwa hata nasi tunataka kombe hili na kushiriki Caf,” akasema Muyoti.

“Tuna kikosi kizuri cha wachezaji, hatuna majeraha na sote tutafanya juu chini kuhakikisha tunatwaa kombe hili,” akaongeza kocha huyo ambaye ni mchezaji wa zamani wa AFC Leopards.

Kocha wa Gor Mahia Zedekiah ‘Zico’ Otieno na nahodha Philemon Otieno nao wameapa kuwa lazima watashinda Nairobi United wala hawatawadharau kwa sababu ni timu ndogo.

“Police wameshinda Ligi Kuu (KPL) nasi matumaini yetu ya mwisho ya kutwaa taji ni kushinda Mozzart Bet. Nairobi United ni timu nzuri na hatutawadharau, tutajituma sana ili kuhakikisha tunacheza soka ya Afrika msimu ujao,” akasema Zedekiah ‘Zico’ Otieno.

Philemon aliwataka mashabiki wa Gor wafike kwa wingi kwenye mchezo huo. K’Ogalo itawakosa mnyakaji Gad Mathews na mabeki Geoffrey Ochieng’ na Kennedy Onyango, wote ambao wapo nje kwa sababu wanauguza majeraha.

Hii itakuwa mara ya kwanza timu hizo zikikutana. Kando na kuwahi fainali ya Mozzart Bet, Nairobi United pia imefuzu kushiriki Ligi Kuu (KPL) msimu ujao baada ya kutwaa ubingwa wa Supa Ligi (NSL).

Kuelekea fainali, timu hiyo imekuwa ikiangusha vigogo na iliwashinda Tusker, KCB, Kakamega Homeboyz na Mara Sugar kwenye raundi ya 32, 16, robo fainali na nusu fainali mtawalia.