Ni kufa kupona Afrika Kusini ikivaana na Canada raundi ya 32 bora
BAADA ya wiki mbili za mechi za hatua ya makundi, macho yote sasa yanaelekezwa kwenye hatua ya mwondoano itakayoanza usiku leo.
Mechi ya kwanza ni kati ya Afrika Kusini na Canada na itawakutanisha washindi wa pili wa Kundi A na Kundi B katika Uwanja wa Los Angeles.
Wengi wanaona ni pambano lisilovutia sana kutokana na makundi hayo kuhesabiwa miongoni mwa timu dhaifu kwenye mashindano haya.
Hata hivyo, wenyeji Canada watakuwa kivutio kikuu licha ya kucheza nchini Marekani mbele ya zaidi ya mashabiki 70,000 katika jiji la Inglewood.
Katika mechi zingine za mwisho za hatua ya makundi, mabingwa watetezi Argentina wataingia uwanjani saa kumi na moja asubuhi dhidi ya Jordan.
Argentina, wanaoongoza viwango vya FIFA, watacheza na Jordan kwa mara ya kwanza katika historia kwenye Uwanja wa AT&T uliopo Dallas. Jordan tayari imeondolewa baada ya kupoteza mechi zake mbili za kwanza.
Wakati huo huo, Algeria watatoana kijasho na Austria. Algeria ilifufua matumaini yake kwa kuichapa Jordan 2-1. Ushindi huo ulikuwa wa kwanza kwa Algeria katika historia ya Kombe la Dunia.
Katika Kundi K, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) itashuka dimbani dhidi ya Uzbekistan kwenye Uwanja wa Mercedes-Benz ikisaka ushindi utakaoiweka katika hatua ya 32 bora. Kwa upande wa Uzbekistan, kushindwa kutamaanisha kuaga mashindano mapema.
Pambano jingine kubwa litawakutanisha vinara wa Kundi K, Colombia na Ureno, kwenye Uwanja wa Hard Rock mjini Miami saa nane asubui ya kuamkia leo.
Colombia inaongoza kundi hilo ikiwa na pointi sita. Sare pekee itatosha kuifanya imalize kileleni mwa kundi. Kwa upande wa Ureno, walio na pointi nne, ushindi pekee ndio utakaowapa nafasi ya kutwaa uongozi wa kundi.