Dimba

Nyota wa Arsenal Emile Smith Rowe atia guu moja Fulham

Na CECIL ODONGO July 27th, 2024 1 min read

ARSENAL wapo tayari kumwaachilia kiungo raia wa Uingereza Emile Smith Rowe ajiunge na Fulham kwenye dili ambayo itagharimu Sh5.9 bilioni.

Smith Rowe, 23, aliuma sana benchi msimu uliopita ugani Emirates na anamakinika kupata klabu ambapo atakuwa akianzishwa mara kwa mara.

Ofa ya Sh5.9 bilioni kutoka Fulham ilikuwa ya kuvutia sana kwa Arsenal ambayo itapata faida pekee kwa sababu mchezaji huyo amekwea ngazi kutoka akademia yao.

Ingawa Crystal Palace pia walikuwa wakimtaka Smith Rowe, Fulham ambayo pia ni timu ya London ilionekana kutimka mbio na sasa inaelekea kumchukua.

Smith Rowe alikosa mechi ya kirafiki dhidi ya Bournemouth iliyosakatwa Amerika ambayo iliishia sare ya 1-1.

Kocha Mikel Arteta alisema Smith Rowe alikosa mechi hiyo kutokana na mjadala unaoendelea kuhusu uwezekano wake mkubwa wa kutua Fulham.

“Kulikuwa na mambo ambayo yamekuwa yakiendelea kichinichini kuhusu uwepo wake klabuni ndiposa tuliamua kumwaacha nje ya kikosi,” akasema Arteta.