Tusker FC kukuwa mwenyeji wa Al Ahli Wad Madani ya Sudan katika mechi ya duru ya pili ya raundi ya kwanza
Tusker FC itakuwa mwenyeji wa Al Ahli Wad Madani ya Sudan katika mechi ya duru ya pili ya raundi ya kwanza ya mchujo wa Kombe la Shirikisho ya Soka Afrika (CAF) leo katika Uwanja wa Nyayo, Nairobi, kuanzia saa tisa alasiri.
Tusker inaingia katika mechi hiyo ikiwa na nafasi nzuri ya kufuzu hatua inayofuata, baada ya kutoka sare ya 2-2 katika mchezo wa kwanza uliochezwa katika uwanja wa Kigali Pele, Rwanda, Jumapili iliyopita.
Mabingwa hao mara 12 wa Ligi Kuu ya Kenya waliongoza 2-0 kabla ya Al Ahli kusawazisha katika kipindi cha pili.
Mshambuliaji wa Nigeria Victor Mbaoma aliipa Tusker bao la kwanza dakika ya 11 kwa penalti kabla ya kuongeza la pili katika muda wa nyongeza wa kipindi cha kwanza. Mabao hayo yalifikisha jumla ya mabao matatu katika mechi tano tangu ajiunge na Tusker akitokea APR ya Rwanda.
Al Ahli ilisawazisha kupitia mshambuliaji Al-Samany Al-Sawi, aliyefunga dakika za 58 na 88.
Kuelekea mechi hii, Tusker wanafaida ya mabao ya ugenini na wanahitaji sare ya aina yoyote ili kufuzu raundi ya pili.
Kocha Julien Mette amewataka mashabiki kujitokeza kwa wingi kuipa sapoti timu hiyo, akisema kucheza nyumbani kutawapa morale ya kupambana.
“Kucheza nyumbani kuna umuhimu wake. Tulishinda Super Cup katika uwanja huu na tunajihisi tuko nyumbani. Itakuwa vizuri sana iwapo mashabiki watajitokeza kutushabikia,” alisema Mfaransa huyo.
Mette pia alithibitisha kuwa beki Warsama Hassan Houssein, ambaye amekuwa nje kwa karibu wiki sita kutokana na jeraha, ataanza benchi. Mlinda lango chaguo la tatu John Mark Otieno yuko nje kutokana na jeraha.
Nahodha Aboud Omar alisema wachezaji wamejifunza kutokana na makosa ya mchezo wa kwanza na wako tayari kupigania ushindi nyumbani.
“Ulikuwa mchezo mgumu ugenini. Tumejifunza kutokana na makosa yetu na Jumamosi tutapigania ushindi,” alisema Omar.
Mshindi wa jumla atafuzu raundi ya pili na ya mwisho, huku ushindi katika raundi hiyo ukimpa nafasi ya kucheza hatua ya makundi.