Kimataifa

Watu 49 wafariki Nigeria baada ya kunywa pombe yenye sumu

Na MASHIRIKA September 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TAKRIBAN watu 49 wamefariki na wengine 182 wamelazwa hospitalini baada ya kushukiwa kuathiriwa na sumu kwenye pombe katika jimbo la Ondo, kusini-magharibi mwa Nigeria, Waziri wa Afya wa jimbo hilo alisema Ijumaa.

Suala hilo liliripotiwa kwa mara ya kwanza Septemba 5, wakati maafisa walisema watu 29 walikuwa wamefariki ndani ya wiki ya kwanza baada ya kunywa pombe hiyo.

Waziri wa Afya wa Ondo, Banji Ajaka, alisema idadi ya waliofariki ilikuwa imeongezeka hadi 49 kufikia Ijumaa.

Mamlaka za Ondo zinashuku kuwa vifo hivyo vilisababishwa na sumu ya methanol iliyokuwa kwenye pombe ya kienyeji inayotengenezwa kwa njia isiyodhibitiwa na inayojulikana kwa jina la “Monkey Tail”.

Tukio hilo limeangazia hatari za pombe zisizodhibitiwa ambazo bado hutumiwa kwa wingi katika baadhi ya maeneo ya Nigeria kutokana na bei yake ya chini na kupatikana kwa urahisi.

Bw Ajaka alisema tukio hilo lilifuatiliwa hadi kwenye sherehe mbili za kitamaduni katika eneo la Odigbo, ambapo wageni walikunywa pombe iliyotengenezwa nchini humo.

“Dalili za ugonjwa na taarifa kuhusu walichokunywa zimeibua tuhuma kubwa za kitabibu kwamba huenda waliathiriwa na pombe yenye sumu. Hata hivyo, bado hatujapata ushahidi wa maabara,” alisema Bw Ajaka katika taarifa.

Waathiriwa waliripoti dalili mbalimbali zikiwemo maumivu ya kichwa, maumivu ya mwili, matatizo ya kupumua, kupoteza fahamu.

Bw Ajaka alisema madhara hayo yalijitokeza kwa kasi baada ya watu kutumia pombe hiyo.

“Jambo hili lilitokea haraka. Unapokunywa, kutegemea kiwango ulichotumia, figo zinaweza kushindwa kufanya kazi, macho kupoteza uwezo wa kuona na ubongo kuharibika,” alisema.

Methanol ni aina ya sumu ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa mwilini inapomezwa.