Dondoo

Ashangaza wanakijiji alipoenda kulilia mtoni eti kidosho hamtaki

Na KALUME KAZUNGU August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

GALOLE, Tana River:

JOMBI alifokewa na wanakijiji baada ya kupatikana amepiga magoti kando ya Mto Tana huku akiomba mamba wajitokeze kumvuta majini asione mrembo akiolewa na mtu mwingine.

Alisema alikuwa amechoka kuumizwa moyo na mpenzi wake na akaona afadhali kumezwa na mamba.

“Afadhali mamba wanimeze. Kwa nini nimpende kwa moyo wangu wote, lakini mwishowe ananivunja moyo?” aliangua kilio akisema hataki kuona demu huyo akiolewa na dume lingine.

Wanakijiji waliompata walimsuta kwa kuthamini mapenzi kama maisha.

“Kaka, maisha ni muhimu kuliko mapenzi au chochote kile. Usife moyo. Cha msingi ni kwamba ukiwa hai mambo yatajipa,” akasikika mwanakijiji akimshauri.

Jamaa huyo aliendelea kulia kwa muda kabla kuondoka hapo akifuata wanakijiji waliokuwa wakimpa moyo.