Habari Mseto

Fyata mdomo, Sakaja amfokea Atwoli kwa kukosoa mabadiliko ya Housing Levy

Na KEVIN CHERUIYOT June 8th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Nairobi Johnson Sakaja amemshambulia hadharani Katibu Mkuu wa Muungano wa Vyama Vya Wafanyakazi (COTU) Francis Atwoli kuhusu matumizi ya ushuru wa nyumba.

Katika matamshi yake Jumapili, Juni 8, 2025 wakati wa ibada ya kanisa iliyohudhuriwa na Rais William Ruto, gavana huyo alisema Bw Atwoli hakuwa mkweli kwenye ukosoaji wake wa ushuru huo wa kujenga nyumba za gharama nafuu.

“Inashangaza sana kwamba Cotu inaweza kusema kujenga masoko kwa kutumia ushuru wa nyumba ni vibaya. Ikiwa mradi wa nyumba utakamilika na soko lijengwe hapo karibu, kuna shida gani? Familia zinazoishi kwenye nyumba hizo zinahitaji mahali pa kununua vyakula na matumizi mengine. Wale wanaopinga mradi huu wanafaa kuaibika kabisa,” akasema Bw Sakaja.

Alidai kwamba baadhi ya viongozi ambao wanapinga mradi huo wanaishi kwenye majumba ya kifahari ilhali wanapinga ujenzi wa makazi ya wananchi wa kawaida.

Gavana pia alimtaka aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kuruhusu serikali kujenga nyumba za kuinua maisha ya wakazi.

“Ni mwananchi wa kawaida anahitaji hizi nyumba, sio wewe. Kwa hivyo jipe shughuli. Usiingilie kuzuia wakati ni mwananchi anasaidiwa,” akasema.

Malumbano haya yanazidisha uhasama kati ya Gavana Sakaja na Bw Atwoli ambaye awali alikuwa akimtambulisha kama mwanawe kwenye hafla za kitaifa.

Cheche za maneno zilianza wakati Bw Atwoli alimkosoa gavana huyo kwa kuruhusu jiji kujaa uvundo na kuruhusu wachuuzi kuzagaa kila kona.

Ukosoaji huo unadaiwa kumfanya Sakaja kukosa sikukuu ya Leba Dei katika Uhuru Gardens.

Jumamosi, Juni 7, 2025, akimjibu Katibu wa Idara ya Makazi Charles Hinga, Bw Atwoli alisema kwamba Cotu haikuhusishwa kwenye mageuzi ya ushuru wa nyumba.

Bw Atwoli alisema kwamba iwapo serikali ingewaalika kwa mashauriano, Cotu haingekubali kugeuzwa kwa ushuru huo kuelekezwa katika kujenga miundombinu mingine ambayo tayari hutengewa pesa kwenye bajeti.

“Huu mkondo wa kubadilisha matumizi ya ushuru wa nyumba ukiendelea, fedha hizo zitajikuta zikielekezwa kujenga barabara, mabwawa na miradi mingine ya bei ghali huku ikiacha wafanyakazi wengi bila nyumba,” akasema Atwoli.