Habari Mseto

Ilani ya ubomoaji yatolewa kwa wenye majumba

October 19th, 2018 1 min read

Na BERNARDINE MUTANU

SERIKALI ya Kaunti ya Nairobi imetoa ilani ya ubomoaji wa nyumba katika mtaa wa Eastleigh.

Katika notisi hiyo iliyoandikwa Jumatano, wamiliki hao wa nyumba za Nyayo Wards, walipewa siku saba za, kutoka siku ya kutolewa kwa ilani hiyo, kubomoa nyumba hizo.

Wamiliki walishutumiwa kwa kujenga bila ruhusa kutoka kwa serikali ya kaunti, “Mnaagizwa kusimamisha ujenzi zaidi na kuondoa nyumba mlizojenga,” ilisema notisi hiyo.

Kulingana na serikali hiyo, ujenzi huo ni kinyume cha sheria za mipangilio ya jiji. Serikali hiyo ilitoa ilani hiyo licha ya kuwa watu tayari wanaishi ndani ya nyumba hizo.

Wamiliki waliepwa siku 14 kukata rufaa ikiwa wana malalamishi yoyote. Katika juhudi za kusafisha jiji la Nairobi serikali imekuwa ikibomoa majumba, hasa yaliyojengwa kando ya mito na maeneo chepechepe pamoja na hifadhi za barabara.