• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:50 AM
Itikadi zazuia wengi kuchukua bima ya mazishi wakiwa hai

Itikadi zazuia wengi kuchukua bima ya mazishi wakiwa hai

Na MWANDISHI WETU

LICHA ya kauli kuwa kuzaliwa ni bahati kufa ni lazima, jamii nyingi barani Afrika bado hazitaki kujadili wazi uwezekano wa mtu kufa kutokana na itikadi na mila ambazo zimepitwa na wakati.

Baadhi ya jamii nchini bado zinaamini kutaja ama kuwazia kifo ni hatua ya kishirikina au kujitakia mkosi, na ndio maana watu wengi wanaachia jamaa zao mzigo mkubwa wa kuwazika badala ya kujipanga mapema.

Miaka ya hivi karibuni, kampuni za bima humu nchini zimezidi kuongeza bima ya kuwafadhili watu pesa za gharama za mazishi wakati wanapokufa.

Hata hivyo, hatua yao hii imekumbana na kibarua kigumu cha kuwaeliwisha Wakenya umuhimu wa kuchukua bima hii, bila kukinzana na itikadi za jamii nyingi zisizokaribisha mjadala kuhusu uwezekano wa kifo.

Kampuni hizo zinajaribu kuwapigia hesabu Wakenya kuwa pale mtu anapokufa, badala ya kusumbua familia na majirani kwa michango ya pesa ili kufanikisha mazishi, mtu anaweza kuhifadhi pesa kidogokidogo nao kisha pale atakapofariki kampuni itoe pesa za kugharamia mazishi yake.

Hadi sasa, kampuni 22 kati ya 26 za bima zimeongeza bima ya kufadhili gharama za mazishi na matukio ya baada ya kifo kwa jumla, kama mbinu nyingine ya kupanua soko. Bima hizi zinahusisha mtu kugharamiwa malipo ya mochari, kununuliwa jeneza, maua, mipango ya mazishi na chakula.

Japo bima zimepewa majina tofauti kulingana na kampuni na mengine yakiwa ya kuvutia, ujumbe ni mmoja tu, kuwa siku moja utakufa na hivyo unahitaji kuanza kuweka akiba itakayokufaa wakati huo. Kampuni hizo zinaahidi kulipa pesa hizo kati ya saa 48 za kupigwa kwa ripoti kuhusu kifo cha mteja wao.

“Tunafahamu kuwa bidhaa hii ya bima ya kifo bado ina mwendo mrefu hapa Kenya. Lakini angalau imekubalika na ‘Chamas’ kwa ajili ya wanachama wao na hiyo ni ishara njema,” Bw Tom Gitogo, Afisa Mkuu Mtendaji wa CIC Insurance.

You can share this post!

JAMVI: Kalonzo atakiwa aombe radhi waasi

Kipusa taabani kuuza mali apate hela za mganga

adminleo