• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 4:55 PM
Machifu kupokea mafunzo ya kijeshi

Machifu kupokea mafunzo ya kijeshi

NICHOLAS KOMU na PETER MBURU

MACHIFU takriban 3,400 na manaibu wa makamishna wa kaunti 440 watahudhuria mafunzo ya lazima ya polisi katika kipindi cha miezi sita ijayo, ili maafisa wa polisi wanaowalinda wapewe majukumu mengine.

Wariri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’I alisema hivyo wakati wa mkutano na viongozi hao wa utawala Jumanne, akisema mafunzo hayo yataongozwa na Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS)

Dkt Matiang’I alisema kila afisa wa serikali kama chifu ama naibu wa kamishna wa kaunti ambaye hajahudhuria mafunzo ya polisi sharti atapitia mafunzo hayo, kama mbinu mojawapo ya kuboresha huduma na kupunguza mzigo kwa kuondoa maafisa wa polisi wa AP wanaowahudumia.

“Tutahakikisha kuwa manaibu kamishna wa kaunti wote na machifu ambao hawajapitia mafunzo ya kivita wanafanya hivyo katika kipindi cha miezi sita ijayo,” akasema waziri huyo.

Mafunzo hayo sasa yameonekana kama mpango unaooana na mabadiliko mapya yanayoendelezwa katika huduma ya polisi, ambayo yatawafanya maafisa wa AP ambao mbeleni walihudumu katika afisi za machifu wakiondolewa.

Vilevile, ni badiliko linalokuja wakati kumekuwepo visa vya mavamizi dhidi ya viongozi hao wa utawala wakati wawapo kazini.

Katika kipindi cha miezi minne, machifu wawili wameuawa kaunti za Nyeri na Turkana wakiwa kazini

“Tunataka kufanya kazi kwa mpangilio tunapoiendesha serikali kuu. Lengo letu ni kutoa huduma bora,” akasema Dkt Matiang’i.

Hatua hii aidha itawasaidia maafisa hao kuwa wakifanya kazi ya kuwa macho ya serikali ya kitaifa, kwani watakuwa wakiripoti kuhusu hali ya miradi inayoendeshwa, na ile iliyokwama kwa wizara ya usalama wa ndani, bila ya kujali mradi unaendeshwa na wizara gani.

“Washirikishi wa kanda huendesha shughuli za serikali katika kanda na hiyo inafaa kuwa hivyo tu tunapoteremka hadi kwa machifu,” akasema.

You can share this post!

Kipchoge na Chepkoech watawazwa wanamichezo bora Septemba...

MAJI MURANG’A: Wa Iria motoni kwa kudharau kamati ya...

adminleo