• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Machifu wakosa afisi, wachapa kazi chini ya miti

Machifu wakosa afisi, wachapa kazi chini ya miti

Na SAMUEL BAYA

BAADHI ya machifu katika kaunti ya Kilifi hawana afisi na wanaendesha shughuli zao chini ya miti.

Jambo hilo limekuwa kero kubwa kwa baadhi ya machifu hao ambao wanajaribu kila hali kuhudumia wakazi wanaofurika chini ya miti hiyo kusaka huduma.

Chifu wa lokesheni ndogo ya Chapungu, eneobunge la Ganze, Bw Nickson Mapenzi, ni mmoja wa wasiokuwa na afisi.

Kila asubuhi, Bw Mapenzi huhudumia wakazi wa Chapungu chini ya mti aina ya mkonga.

“Haya ndiyo maisha yetu tukifanya kazi za serikali. Hakuna afisi hapa na nimejaribu kwa muda mrefu lakini bila mafanikio. Tumejaribu kutuma maombi lakini bado hatujafaulu,” akasema Bw Mapenzi.

Hata hivyo licha ya kutekeleza kazi hiyo, changamoto alisemani nyingi.

“Nimefanya kazi hii huu ni mwaka wangu wa 10. Sijawahi kuona afisi na kivuli hiki ndiyo afisi ambayo ninatumia kila siku,” akasema huku akiendelea kuwahudumia wananchi.

Aidha chifu huyo alisema kuwa mara nyingi shida ambazo zinamkumba ni kuwa wakati wa mvua, hana mahali pa kuficha stakabadhi muhimu za serikali hivyo kazi hukwama.

“Ujue kivuli hiki ndio afisi ya umma na kila kunaponyesha siwezi kuja kwa sababu nitaharibu karatasi hizi,” akasema.

Wakazi wa kijij hicho cha Chapungu walitoa ardhi hiyo miaka kadhaa iliyopita ili kumwezesha chifu huyo kupata afisi lakini kwa sasa imeshindikana na hali alisema huenda ikaendelea hivyo.

“Jamii ya hapa ilitoa ekari mbili za ardhi ili kujenga afisi ya chifu mdogo lakini bado zoezi la ujenzi. Nasubiri kwa sababu tayari tumetoa mapendekezo yetu kwa mbunge na sasa tunasuburi,” akasema.

Katika lokesheni ya Bandari, hali ni hiyo hiyo. Katika kituo cha biashara cha Bandari, chifu Julius Mwalimu pia hana afisi.

“Nilikuwa na afisi ndogo ya matope lakini ikaharibiwa na mafuriko miaka minne iliyopita. Siku hiyo stakabadhi zote za serikali zililoa maji na hadi leo bado sijapata afisi,” akasema Bw Mwalimu.

Na ili kuwahudumia wananchi afisa huyo alisema kuwa wanakaa chini ya mti ama wakati wa mvua, huwa wanaomba chumba katika kijiji jirani ili kuwahudumia wananchi.

“Hali ni mbaya lakini tunasukumana tu hivyo. Wakati wa mvua tunaomba chumba hapa kijijini. Tunasubiri kumuona mbunge ili atueleze kuhusu changamoto ambazo tunapitia,” alisema.

Aidha chifu huyo alisema kuwa manaibu wa chifu katika lokesheni zake nne hawana afisi na wanahudumu chini ya miti.

Naye chifu mdogo katika lokesheni ya Mwakwala, Bw Henry Shujaa alisema kuwa tangu aajiriwe kama naibu wa chifu mwaka mmoja uliopita, bado hajaona afisi.

“Hata yule mtangulizi wangu alikuwa akiwahudumia wakazi wa Mwakwala akiwa chini ya mti.

Tumejaribu kuomba ufadhili lakini hali inaonekana bado. Tuko na shida sana kwa sababu wakati wa mvua, kazi huwa inakwama,” akasema Bw Shujaa.

Katika kata ndogo ya Nambani iliyoko katika lokesheni ya Mtsara Wa Tsatsu, chifu Margaret Baya pia hana afisi. Hii ni baada ya afisi ndogo ya matope ambayo alijengewa na wananchi kubomoka.

“Sasa kila jioni, mimi hubeba stakabadhi za serikali hadi nyumbani. Afisi yangu ni chini ya mti na ninaomba tu kama kuna mtu anaweza kujitolea kunijengea afisi. Wananchi wanajaribu lakini kwa sababu ya hali ngumu za kimaisha, hawajaweza kunijengea afisi,” akasema.

Akongea na Taifa Leo baada ya kuzuru vijiji vya Chapungu, Jila, na Bandari mbunge wa Ganze Bw Teddy Mwambire alikiri kuwa machifu wengi hawana ofisi na kusema kuwa kuanzia mwakani, juhudi za kuanza kuwajengea maofisi zitaanza.

“Hii ni shida ambayo ilianza zamani kwa sababu wengine wamefanya kazi hadi wamestaafu bila kuona afisi. Lakini kwa sasa tunataka kubadlisha mfumo na mambo yawe tofauti.

Tunapania kuhakikisha kwamba tunatenga fedha mwakani tuanze. Hatuwezi zote kuzijenga ila naamini tunaweza kuanzia mahali,” akasema Bw Mwambire.

You can share this post!

Hoteli ya DusitD2 hatimaye yafunguliwa tena kwa umma

Pasta atimua polo kumtamani bintiye kanisani

adminleo