• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Ndege waharibifu walivyoangamizwa Mwea

Ndege waharibifu walivyoangamizwa Mwea

Na George Munene  

MAMILIONI ya ndege aina ya quelea ambao wamekuwa wakitatiza wakulima wa mpunga katika shamba kubwa la Mwea, Kaunti ya Kirinyaga, wameangamizwa.

Serikali kuu ikishirikiana na ile ya kaunti inayoongozwa na Gavana Anne Waiguru ilinyunyiza dawa baada ya maelfu ya wakulima kulalamika wakihofia hasara.

Naibu Gavana Peter Ndambiri alisema hatua ilichukuliwa baada ya idara ya kilimo katika kaunti kufanya upelelezi kwa wiki kadhaa.

“Wakati wakulima walipolalamika kuhusu uvamizi wa ndege hao katika mashamba yao, maafisa wetu walianza kuchunguza mienendo ya ndege hao hadi kutambua tundu zao. Walinyunyiziwa dawa kwa siku mbili mfululizo kwa hivyo sasa wakulima watarajie mavuno mengi,” akasema Bw Ndambiri.

Wakulima walisifu hatua hiyo na kusema kama ndege hawangeangamizwa, mazao yao yote yangeharibiwa msimu huu.

Ndege hao wadogo huorodheshwa kuwa miongoni mwa waharibifu zaidi mashambani kwani huweza kula hadi gramu kumi za nafaka kila mmoja kwa siku.

You can share this post!

Seneta akemea wanaomhepa Ruto

Watahiniwa wa KCSE wakubali kuhamishwa

adminleo