Habari Mseto

Polisi wajeruhiwa na mwendawazimu kwenye operesheni

October 24th, 2018 1 min read

John Njoroge Na Macharia Mwangi

ASKARI wawili wa kitengo cha kukabiliana na wizi wa mifugo walijeruhiwa baada ya kushambuliwa na mwanamume mwenye matatizo ya kiakili eneo la Elburgon, Kaunti ya Nakuru.

Maafisa hao wanaohudumu katika shamba la Cheponde, Elburgon, walishambuliwa kwa panga na mgonjwa huyo maafisa hao walipoenda kumsaidia jirani aliyeomba usaidizi.

“Mmoja wa maafisa hao alikatwa mkononi,”alisema mkazi mmoja.

Wauguzi katika hospitali ya wilaya ya Elburgon walisema afisa huyo alipata majeraha mabaya mkononi.

Katika kisa kingine eneo la Gilgil, polisi wanachunguza kifo cha mwanamume ambaye mwili wake ulipatikana ukining’inia ndani ya nyumba ya familia eneo la Elementaita. Mkuu wa polisi wa eneo hilo (OCPD) Emmanuel Opuru alisema uchunguzi wa awali ulionyesha mtu huyo alijitia kitanzi.

Hata hivyo alisema haikubainika mara moja kilichomsukuma mwanamume huyo kujitoa uhai. “Marehemu hakuacha ujumbe kueleza sababu ya kujiua lakini tunachunguza,” alisema.