• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 3:07 PM
Seneta Linturi apambana mahakamani kuhusu digrii

Seneta Linturi apambana mahakamani kuhusu digrii

Mawakili Profesa Tom Ojienda (kulia), James Orengo na Seneta Mithika Linturi wakiwa na watu wengine kortini Machi 21, 2018. Picha/ RICHARD MUNGUTI

Na RICHARD MUNGUTI

SENETA wa Meru Mithika Linturi Jumatano alipambana katika Mahakama Kuu kufa kupona aruhusiwe kuhitimu digirii ya uzamili katika somo la Uanasheria.

Jaji George Odunga aliombwa akishurutishe Chuo Kikuu  cha Nairobi (UoN) kimkubalie ahitimu huku Bw Linturi akisema jina lake liliondolewa katika orodha ya mahafala mnamo Desemba 22, 2017 na “kumuaibisha sana.”

Mwanasiasa huyo anayewakilishwa na mawakili wenye tajriba ya juu Seneta James Orengo na Profesa Tom Ojienda alisema hakupewa fursa ya kujitetea dhidi ya madai kwamba alikuwa ameghushi digrii ya kwanza kutoka chuo kikuu kimoja cha ng’ambo.

Bw Linturi alisema UoN kilimdhihaki pakubwa kilipoondoa jina lake katika orodha ya mahafala dakika ya mwisho.

“Wakufunzi wa Bw Linturi walisema alikuwa amepita mitihani na kuidhinishwa kisha jina lake likachapishwa katika orodha ya waliohitimu,” alisema Prof Ojienda.

Wakili  huyo aliwasilisha mbele ya Jaji Odunga karatasi za mitihani iliyokuwa imesahihishwa na kuomba mahakama ifutilie mbali uamuzi wa kumzuia Bw Linturi kuhitimu.

Mawakili Orengo na Prof Ojienda waliwasilisha risiti za kuonyesha jinsi Bw Linturi alikuwa amelipa karo na  kutimiza masharti yote ya chuo kikuu.

Lakini wakili Donald Kipkorir anayekitetea chuo hicho cha UoN, Tume ya Kupambana na Ufisadi nchini (EACC), afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) alipinga kesi ya Bw Linturi  na kusema hatua ya kuondoa jina la mwanasiasa huyo kutoka kwa orodha ya mahafala ilifaa.

“UoN kilipashwa habari za kutohitimu kwa Bw Linturi alipokuwa akisoma ng’ambo kabla ya kukubaliwa kuendelea na masomo ya juu humu nchini,” alisema Bw Kipkorir.

Wakili huyo alimsihi Jaji George Odunga atupilie mbali kesi ya Bw Linturi kwa vile alifukuzwa kutoka chuoni na ‘sio mwanafunzi tena wa Chuo Kikuu cha Nairobi.”

Bw Kipkorir alieleza korti kwamba ufisadi ukiguduliwa hatua huchukuliwa na “hivyo ndivyo UoN kilifanya kilipofahamishwa na EACC na IEBC kuhusu vyeti vya mlalamishi.”

Kiongozi wa mashtaka kutoka afisi ya DPP Ashimoshi Shitambashi aliomba Jaji Odunga  atupilie mbali ombi la Bw Linturi la kuzuia akichukuliwa hatua ya kisheria ikiwa ni pamoja na kushtakiwa.

EACC na IEBC ziliomba korti iruhusu sheria ifuate mkondo na hatua ichukuliwe dhidi ya Bw Linturi.

Jaji Odunga atatoa uamuzi Aprili 25, 2018.

You can share this post!

Wakazi wa Githurai 45 waiomba mahakama imwachilie polisi...

Gor kukabana na SuperSport United Confederations Cup

adminleo