• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Thiwasco yashirikiana na kaunti kuweka vituo vya usafi Thika

Thiwasco yashirikiana na kaunti kuweka vituo vya usafi Thika

Na LAWRENCE ONGARO

WANANCHI mjini Thika wameanza kuzingatia hali ya usafi kwa kunawa mikono kila mara baada ya vituo vitano vya kunawa mikono kuwekwa.

Kampuni ya Thiwasco Water Company Ltd imezindua mikakati ya kuwawekea watumiaji vituo vitano vya kunawa mikono kwa juhudi za kukabiliana na COVID-19.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bw Moses Kinya amesema hiyo ni njia mojawapo ya kuwapa wananchi matumaini ya kukabiliana na COVID-19.

“Kampuni yetu imechukua hatua hiyo kwa ushirikiano na Kaunti ya Kiambu, ili tuweze kupambana na COVID-19,” amesema Bw Kinya.

Amesema maafisa wake wameweka vituo hivyo katika maeneo tofauti mjini Thika ambako watu wengi hujumuika.

Eneo la kwanza ni katika hospitali kuu ya Thika Level Five ambapo kuna mifereji miwili ya maji safi ya kutumika wakati mtu ananawa na kusafisha mikono.

Kituo cha pili ni katika kituo cha Polisi cha Thika.

Halafu Soko kuu la Jamhuri kuna mifereji na pia katika lango kuu la kuingia kampuni ya Thiwasco Water Company Ltd.

Janga la COVID-19 limegeuza mawazo, tabia na mienendo ya wananchi kuhusu usafi huku kila mahali pa biashara watu wakiwekewa jeli spesheli ya kunawa mikono ambayo inaua viini.

Maeneo yanayozingatia usafi kamili ni mikahawa na kweye maduka.

Wakazi wengi waliohojiwa wamepongeza juhudi za kampuni ya Thiwasco Water Company Ltd kwa kuletea watu maji kwa wingi katika kila kona.

“Tumefurahia hatua hiyo kwani kila mmoja atajichunga mwenyewe kwa kunawa bila kulazimishwa. Hiyo ni njia moja ya kuzingatia usafi,” amesema Bw Peter Macharia ambaye ni mkazi wa Thika.

Kutokana na janga hilo la COVID-19 kila mwananchi yuko chonjo ambapo hakuna yeyote angetaka kuchezea afya yake.

Hata ingawa sio matatu nyingi zinazingatia kunawisha wasafiri lakini wengi wa wasafiri wanaonekana kufungua madirisha wakiingia katika matatu.

“Mimi ninapoingia ndani ya matatu ninahakikisha kuwa ninafungua dirisha ili hewa safi iingie. Sasa hakuna kuleta mchezo kwa sababu jambo hili ni hatari,” amesema John Kimani ambaye alikuwa kwenye matatu moja ya kutoka Thika kuelekea Ruiru.

Uchunguzi uliofanywa umebainisha ya kwamba jeli ya kunawa – Sanitiser – imepungua sana katika supamaketi baada ya wateja wengi kununua kwa fujo.

Imebainika kuwa hakuna mwananchi yeyote anayechukua jambo hilo kwa mzaha kwa sababu kila mara mtu anatamani kunawa mikono.

You can share this post!

Ofisi kadhaa za serikali zafungwa mjini Thika

CORONA: Wauzaji miraa wakemea marufuku

adminleo