Habari Mseto

Vuguvugu lataka Bunge kubadilisha muundo wa fimbo ya mamlaka  

March 4th, 2024 1 min read

NA WANDERI KAMAU

VUGUVUGU moja linataka Bunge na Seneti kuandaa vikao vya umma kujadili muundo wa fimbo za mamlaka (maces), ambazo zimekuwa zikitumika katika mabunge hayo tangu uhuru.

Vuguvugu hilo, linaloitwa

Kupitia mshirikishi wake mkuu, Bw David Kimengere, linadai kuwa muundo wa fimbo hizo unafanana na rungu, ambayo ni ishara ya vita.

“Tunafahamu kuwa kulingana na historia, fimbo ya mamlaka ilikuwa silaha ya kumlinda Mfalme wa Uingereza hadi katika karne ya 14. Kuna visa ambavyo vimerekodiwa ambapo fimbo hiyo ilikuwa ikitumika kuwagonga watu vichwani,” likaeleza vuguvugu hilo.

Pia, linataka Bunge kutoa ufafanuzi wa wazi kuhusu madai kuwa, baadhi ya alama zilizo katika fimbo hiyo ni za kishetani.

Kutokana na hayo, linalitaka Bunge kuandaa vikao vya umma ili kubadilisha muundo wa fimbo hizo ili “kuwiana na tamaduni na desturi za Wakenya”.

Hata hivyo, Bunge limesema kuwa baada ya kutathmini ombi lililotumwa kwake na vuguguvu hilo, “litashughulikia hayo kupitia taratibu zake za ndani”.

“Bunge huwa linaendesha shughuli zake kwa kuzingatia desturi, kanuni na taratibu. Baada ya kutathmini ombi lako, tumeamua litashughulikiwa kupitia michakato na taratibu za ndani za Bunge,” akasema Msajili wa Bunge, Bw Samuel Njoroge, kwenye barua aliyotumia vuguvugu hilo.