• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Wasiwasi wanawake wengi kujihusisha na ugaidi

Wasiwasi wanawake wengi kujihusisha na ugaidi

Mkewe Sheikh Aboud Rogo aliyeuawa, Hania Sagar, akiwa katika mahakama ya Shanzu, Mombasa Februari 16, 2018. Sagar alihukumiwa kifungo cha miaka 10 jela na hakimu Diana Mochache kuhusiana na ugaidi. Picha/ Maktaba

Na MOHAMED AHMED

TARKIBAN wanawake 13 ni ama wanatumikia kifungo, wamewahi kuzuiliwa katika gereza la Shimo La Tewa au wameachiliwa baada ya kupatikana na makosa ya kujihusisha na ugaidi.

Ufichuzi huu unakuja huku maafisa husika wakieleza wasiwasi kuhusiana na ongezeko la wanawake kujiunga na makundi hayo ya kigaidi.

Katika uchunguzi wa Taifa Leo tumekusanya idadi hiyo ya wanawake ambao wamewahi kukamatwa baada ya kuhusika na ugaidi.

Mnamo Septemba 11 mwaka 2016 kituo cha polisi cha Central jijini Mombasa kilivamiwa na magaidi.

Magaidi hao walikuwa ni wanawake walioweza kuwaua maafisa wa usalama. Kuhusika kwa wanawake hao katika shambulizi hilo kulipelekea kufichuka baina ya idara za usalama kuwa wanawake wamekuwa katika msitari wa mbele katika makundi ya kigaidi.

Wanawake hao wanaojiunga na makundi hayo ikiwemo Al shabaab wanasemekana kuhusika na kufanya kazi kama vile upishi na kuwa majasusi wa makundi hayo.

Miongoni mwa wa wanawake ambao wanatumikia vifungo kufuatia kuhusika kwao na ugaidi ni pamoja na mke wa imamu aliyeuawa Aboud Rogo, Bi Hania Sagar na Bi Mwanasiti Masha ambaye ni mke wa aliyekuwa mwanajeshi.

Bi Sagar anahudumu kifungo cha miaka 10 huku Bi Masha akihudumu kifungo cha miaka saba katika gereza hilo la Shimo la Tewa.

Wanawake wengine watano ambao wamewahi kushtakiwa kwa mashtaka yanayohusiana na ugaidi ni Ummulkheir Sadri Abdalla, Khadija Abubakar Abdulkadir, Maryam Said Aboud, Halima Adan na Feruz Abubakar Hamid.

Watano hao wapo nje baada ya kuachiliwa kwa dhamana na kesi zao zinaendelea na zitasikizwa mwezi Machi.

Ummulkheir Sadri Abdalla, Khadija Abubakar Abdulkadir, Maryam Said Aboud na Halima Adan walishtakiwa mnamo mwaka 2015 baada ya kukamatwa kwa madai kuwa wanaenda kujiunga na kundi la Al Shabaab.

Bi Hamid alikamatwa eneo la Bondeni Mombasa baada ya kupatikana na vilipuzi. Katika mahojiano Bi Khadija ambaye ni mmoja ya wanawake hao alisema kuwa kesi yao imekuwa ikienda polepole hata hivyo alisema kuwa yupo na matumaini ya kuachiliwa huru.

 

You can share this post!

Mswada wa Waziri Mkuu mwenye mamlaka kuliko Rais...

Uchomaji makaa wapigwa marufuku Narok

adminleo