• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 5:01 PM
Wazee wa Kaya walaumiana kwa kuunga mkono MRC

Wazee wa Kaya walaumiana kwa kuunga mkono MRC

Na SIAGO CECE

Makundi ya wazee wa Kaya Mzirima na Mzidia yamedai kuwa Kaya Bombo imewaficha wanachama wa kundi la MRC (Mombasa Republican Council), jambo ambalo limefanya maafisa wa usalama waingilie kati.

Akizungumza na Taifa Leo, Mzee Mkoba Gwashe anayewakilisha wazee wa Kaya Rabai, hata hivyo, alipinga madai hayo na kusema hatua ya polisi kuwataka kuripoti kwenye kituo kabla ya kuzuru kaya zao inakiuka haki zao za kuabudu.

Hata hivyo, Wazee wa Kaya Bomba kwa upande wao wamejitokeza kwa kusema madai hayo si ya kweli kwani hawana uhusiano wowote na kundi hilo la MRC.

Wakiongozwa na Mzee Gwashe, walisema kuwa tayari wana mipango ya kuenda kortini ili kutatua ugomvi wao.

“Bado tunatafuta wakili atakayetuwakilisha kortini, si sawa polisi kutuagiza kupiga ripoti kwenye kituo ilhali haya ni masuala ya mila yetu,” alisema.

Alieleza kuwa tatizo hilo lilianza mwanzoni mwa mwaka huu ambapo wazee walienda kufanya matambiko msituni kama ilivyo desturi yao kila mwaka.

Lakini Naibu kamishna wa Kaunti ya Kilifi, Bw Jama Mohamud alisema wazee hao walikuwa na tofauti zao hivyo basi suala la MRC si la kweli.

“Hatujaona vijana wowote wa MRC, hizi tu ni tofauti ambazo wazee wanazo zinazowafanya kulaumiana. Nimewapa wiki mbili ili kutatua suala hilo pamoja na machifu,” alieleza Bw Jama.

Amri hiyo ya wiki mbili ilitolewa baada ya kamishna huyo pamoja na mafisa wengine wa polisi, machifu na wazee wa kaya kufanya mkutano wa dharura.

“Tunaelewa kuwa wazee hawa ni muhimu sana katika jamii na wanasaidia kutunza misitu hii. Kukiwa na jambo kama hili ni bora kulitatua mapema,” alisema Bw Jama.

Bw Jama pia alisema wamefanya mpango wa kuomba usaidizi kutoka kwa Shirika la Uhifadhi wa Misitu (KFS) kulinda misitu ya Kaya dhidi ya kuvamiwa.

Kundi la MRC liligonga vichwa vya habari katika miaka ya hivi majuzi baada ya kuanzisha mchakato wa kutenga eneo la Pwani kama sehemu inayojisismamia, lakini serikali ililiharamisha.

You can share this post!

Si lazima niwe Rais 2022 – Raila

Wandani wa Ruto waingia baridi

adminleo