• Nairobi
  • Last Updated May 6th, 2024 2:59 PM
Wizara yawataka watalii waepuke mitego ya matapeli mitandaoni

Wizara yawataka watalii waepuke mitego ya matapeli mitandaoni

Na MAGDALENE WANJA

WIZARA ya Utalii na Wanyamapori imeanzisha uchunguzi kuhusu ripoti za watu ambao wanawalaghai watalii mitandaoni.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotiwa sahihi na mkurugenzi wa mawasiliano wa wizara hiyo Bw Mulei Muia, kuna visa vingi vya ulaghai ambavyo vimeripotiwa katika ofisi za wizara hiyo.

Kulingana na habari hiyo, walaghai hao hawana kibali cha kufanya kazi wala ofisi zozote.

“Utafiti wa hivi punde unaonyesha kwamba wahudumu hao walaghai hawana leseni kutoka kwa mamlaka ya kudhibiti shughuli za utalii (TRA) na wala ya kutoka kwa muungano wa wahudumu wa kitalii wa Association of Tour Operators (Kato),” inasema taarifa hiyo.

Habari hiyo pia inasema kuwa uchunguzi tayari umeanzishwa na washikadau mbalimbali katika sekta ya utalii.

“Hata hivyo, tunawataka watalii wote wa humu nchini na wale wa kutoka nje kuwa makini sana wanapotumia mitandao kutafuta sehemu za kutembelea ili kujikinga dhidi ya walaghai. Tunawashauri kutembelea tovuti maalum kama vile htts://www.tourismauthority.go.ke.”

Haya yanajiri siku mbili baada ya habari zilizofichua jinsi watalii wengi wanaotembea humu nchini hujipata taabani baada ya kulaghaiwa mitandaoni.

Waziri wa Utalii na Wanyamapori ni Najib Balala (pichani).

You can share this post!

Walimu waitaka serikali kuu kutwaa usimamizi wa elimu ya...

Mhadhiri mpenda lugha mama na aliye na historia pevu

adminleo