Habari Mseto

Elimu imefanya wizi wa mifugo kupungua, Lonyagapuo asema

June 23rd, 2019 1 min read

Na Oscar Kakai

Gavana wa Kaunti ya Pokot Magharibi, Profesa John Lonyangapuo, amesema kuwa visa vya wizi wa ng’ombe katika eneo hilo vimepungua kwa sababu vijana wengi huenda shule.

“Mungu ni mwema, sasa visa vya wizi wa ng’ombe vimepungua pakubwa, tunataka wazazi wasilegeze kamba kwa kupeleka watoto shule,” alisema.

Profesa Lonyangapuo alisema kuwa shule nyingi zimefunguliwa katika eneo hilo huku akiwaomba wakazi kukumbatia elimu.

“Tumejaribu kufungua shule katika kila kijiji ili kupunguza maovu.Vijana wengi sasa wamekombolewa na wameacha wizi,” alisema. Gavana huyo alihimiza jamii za Pokot ,Turkana na Marakwet kuacha mizozo huku akisema hali hii imerudisha nyuma elimu na maendeleo.

Profesa Lonyangapuo alisisitiza kuwa ni lazima kuwe na amani kati ya jamii hizo ili eneo hilo liweze kustawi.

Kiongozi huyo aliwataka viongozi wa jamii hizo kukoma kuwachochea wananchi huku akiwarai wakazi kuwa na umoja.