Gachagua aapa kuzima njama za kuleta mgawanyiko Mlimani
KIONGOZI wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, ameapa kupinga kile alichokitaja kama njama za Rais William Ruto kugawanya eneo la Mlima Kenya kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Akizungumza katika mikutano ya hadhara mjini Embu, Kathangariri, Karurumo, Gategi na Siakago Jumamosi, Gachagua alimshutumu Rais Ruto kwa kutumia Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku kuendeleza mpango wa kugawanya eneo hilo kuwa Mlima Kenya Mashariki na Magharibi.
“Lazima nimzuie Ruto kugawanya Mlima Kenya. Tunataka tubaki pamoja ili tumpeleke nyumbani katika uchaguzi ujao,” alisema Gachagua katika soko la Kathangariri, Embu.
Alidai Rais Ruto amewasaliti wakazi wa Mlima Kenya waliomuunga mkono kwa wingi 2022 kwa kuwaita wakabila.
Pia alimshutumu Rais kwa madai ya kuruhusu makundi ya wahuni kuwashambulia wakazi wa Mlima Kenya na kuharibu mali yao.
“Nitahakikisha Ruto anakuwa rais wa muhula mmoja. Kilichotokea Ol Kalou kitajirudia katika Mlima Kenya mzima,” alisema.
Gachagua pia alimkosoa Waziri wa Afya Aden Duale kwa madai ya kutoa matamshi ya kuwadhalilisha wakazi wa Mlima Kenya, akisema atawajibishwa kisiasa katika uchaguzi ujao.